
KLABU ya Manchester United ipo katika mikakati ya kuutanua Uwanja wa Old Trafford katika upande wa majukwaa ili kuingiza watu 88,000 kutoka 75,000 wanaoweza kupata siti kwa sasa.
Hivi karibuni Kocha wa United, Jose Mourinho alilalamika kuwa mashabiki wao wanakuwa kimya wakati wa mchezo kitu ambacho hafurahishwi nacho, hivyo ikiwa ongezeko hilo litafanyiwa kazi, watakuwa na nafasi kubwa ya kuongeza mashabiki wao wakati wa mechi.

Ripoti ya kuanza kwa mradi huo bado ipo chini ya uongozi lakini hata kama ukifanyika hautakiwi kuingiliana na mipango ya usajili.
Licha ya kutumia pauni milioni 300 tangu alipotua United, Mei 2016, bado Mourinho amekuwa akisisitiza kuboresha kikosi chake cha sasa, hivyo bajeti ya mambo hayo mawili inatakiwa isiharibu mipango.
Kingine ambacho kinaishawishi United kuboresha uwanja wao ni kutokana na wapinzani wao wakiwemo Man City ambao wameboresha uwanja wao na kuwa na huduma nyingi zaidi.