
MCHEZO wa soka ni biashara kubwa katika mataifa mengi duniani, kuna wachezaji ambao wanalipwa mishahara mikubwa na malipo mengine ya matangazo ya biashara kutokana na vipaji vyao kwenye mchezo huo.
Tanzania tupo katika njia nzuri ya kuelekea katika mafanikio angalau ya kuwa nchi iliyoonyesha mfano wa kuwa na ramani nzuri ya soka, na hiyo inachangiwa na sisi wenyewe kukosoana na kuwa wazi pindi tunapoona kuna mambo hayaendi sawa.
Wakati hali ikiwa hivyo, kumeanza kufukuta mvutano wa ndani ya Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF) baada ya maamuzi ya kufungiwa maisha kwa Michael Wambura ambaye alikuwa Kaimu rais wa taasisi hiyo kubwa ya mchezo wa soka.
Inaweza kuonekana ni kitu kidogo lakini kitendo cha Wambura ambaye alichaguliwa kwa kura nyingi kufungiwa baada ya tuhuma zake kuibuliwa ndani ya muda mfupi, kinaweza kusababisha maswali mengi.
Hoja ni kuwa Wambura kafungiwa kwa makosa yake ya nyuma, imani ya wapiga kura juu yake inaonekana ilikuwa kubwa na ndiyo maana hata ushindi wake ukawa mkubwa, kuondolewa kwake hakuwezi kuchukuliwa kawaida kwa mazingira hayo.
Licha ya kuwa Rais wa TFF, Wallace Karia hakuwa tayari kulizungumzia hilo kwa madai kuwa bado lipo katika mikono ya kamati zenye mamlaka, ni vema uongozi mzima wa TFF ukatazama suala hilo kwa jicho la tatu ili lisije likachangia kuwavuruga wanachama wao na mwisho wake kusababisha mgogoro ni mbaya
kwa afya ya mchezo huo.