The House of Favourite Newspapers

Sonso Achota Sh mil 20 Yanga

IMEFAHAMIKA kuwa beki kiraka mpya wa Yanga, Ally Sonso amekubali kusaini mkataba wa miaka miwili kwa dau la Sh milioni 20 ili akipige Jangwani.

 

Sonso ni kati ya wachezaji wapya 13 waliosajiliwa na Yanga kwa ajili ya msimu ujao wengine ni Farouq Shikalo, Metacha Mnata, Ally Ally, Ally Mtoni, Lamine Moro.

 

Wengine ni Mustapha Suleiman, Patrick Sibomana, Issa Bigirimana, Mapinduzi Balama, Abdulaziz Makame, Maybin Kalengo, Juma Balinya na Sadney Urikhob.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumatatu kutoka ndani ya uongozi wa Yanga, ni kuwa beki huyo amekubali kusaini mkataba kwa kiasi hicho cha fedha baada ya kufikia muafaka mzuri katika dau la usajili ambalo amelihitaji.

 

Mtoa taarifa huyo alisema kuwa, awali beki huyo alikuwa akihitaji shilingi milioni 30 kabla ya kuzungumza na viongozi na kukubali kusaini kwa dau hilo la fedha.

 

“Sonso siyo mchezaji mbaya ni mzuri ana kiwango kizuri anayemudu kucheza nafasi zaidi ya moja katika safu ya ulinzi na kiungo mkabaji namba sita.

 

“Sonso amekubali kusaini mkataba huo baada ya kukubaliana baadhi ya vitu ikiwemo mshahara na dau la usajili ambalo hilo amelitaka yeye,” alisema mtoa taarifa huyo.

 

Alipotafutwa Mwenyekiti wa Yanga, Dk Mshindo Msolla kuzungumzia hilo, simu yake iliita bila ya kupokelewa.

Aidha, Msolla hivi karibuni aliahidi kufanya usajili wa mchezaji yeyote atakayemhitaji kocha katika usajili wao kwa dau lolote.

WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam

Comments are closed.