×

Bashiru Asema ‘Kazi na Bata’ ni Kudhalilisha Wanawake

 

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Bashiru Ally, amewataka wananchi kupuuza kauli ya kufanya kazi na kula bata ambayo imeratibiwa na Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe,  na kusema kauli hiyo itachangia kuzorotesha uchumi wa taifa.

 

Bashiru amesema katika nchi ambayo wananchi wanapambana kujikomboa kiuchumi, hasa katika nchi zetu za Afrika ambazo bado zipo nyuma kimaendeleo ya mtu mmoja-mmoja na taifa kwa ujumla, kutokea kiongozi mmoja kuwaambia watu wafanye kazi kwa starehe ni usaliti mkubwa wa mapambano ya kiuchumi.

 

“Nchi hii ambayo tunaongoza mapambano ya kujikomboa kiuchumi, inamhitaji kila mtu kwa nafasi yake kuhimiza kufanya kazi kwa bidii, na huku CCM kuna kauli mbalimbali za kuhimiza kazi zikiwemo, Hapa Kazi tu, Kazi na Maendeleo, Uhuru na Kazi na Kazi ni Utu, ila kuna baadhi ya vyama wao wanahubiri kazi na starehe, na huo ndiyo utofauti wa chama kiongozi na vyama vya uchaguzi.

 

“Unaposema kazi na bata, maana yake ni kudhalilisha wanawake na mama zetu ambao wakati wote wamekuwa wakifanya kazi kusomesha watoto wao, wakifanya kazi kulisha familia zao, na sote hapa ni matokeo ya juhudi kubwa za mama zetu.

 

“Kuwaambia wale bata, ni sawa na kuwataka washinde kwenye starehe huku watoto wakidhalilika kwa kutokwenda shule.  Hizi ni kauli za kipumbavu za vyama vya uchaguzi, ambazo hatuna budi kuzidharau na kuzipuuza,” amesema.

 

Leave a Comment