

BENKI ya NMB imekabidhi misaada mbalimbali ya vifaa tiba na vifaa vya elimu katika Mikoa ya Dar es Salaam na
Kilimanjaro, ikiwa ni sehemu ya utaratibu wa kurejesha kwa jamii asilimia moja ya faida yao kupitia Programu ya
Uwajibikaji kwa Jamii (CSR).
Jijini Dar es Salaam, NMB imetoa msaada yenye thamani ya Sh. Mil. 15 kwa Shule ya Sekondari Tambaza, iliyopo
Upanga na Kituo cha Afya Pugu Kajiungeni wilayani Ilala jijini Dar es Salaam, wakati Mkoani Kilimanjaro imekabidhi
vifaa tiba kwa Hospitali ya Wilaya ya Hai.
Tambaza Sekondari, imepokea msaada wa vitanda 80 vya kulalia wasichana wa shule hiyo vyenye thamani ya Sh.
Mil. 10, vilivyokabidhiwa na Meneja wa NMB Kanda ya Dar es Salaam, Badru Idd na kupokelewa na Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mussa Zungu.
Katika hafla ya kukabidhi vifaa tiba katika Kituo cha Afya Pugu Kajiungeni, NMB ilikabidhi msaada huo wenye
thamani ya Sh. Mil. 5 kupitia kwa Meneja Mwandamizi wa NMB Kitengo cha Biashara za Serikali, Adelard
Mangombo, na kupokelewa na Mkuu wa Wilaya ya Ilala (DC), Sofia Mjema.