×

Ndege za Kimataifa Zaruhusiwa Kuruka, Kutua Tanzania

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe, akifafanua jambo kwa waandishi wa habari  alipokutana nao kutoa taarifa ya kuruhusu anga la Tanzania kutumika kwa ndege za abiria, biashara na mizigo,  jijini Dodoma.

SERIKALI imefungua anga ya Tanzania, hivyo kuanzia jana Mei 18, 2020 ndege zote za kibiashara, misaada, kidiplomasia, za dharura na ndege maalumu zinaruhusiwa kuruka, kutua na kupita juu ya anga.

 

Hatua hii imechukuliwa kufuatia kufanyika kwa tathmini ya mwenendo wa ugonjwa wa Covid-19 ikiwa ni siku 11 tangu serikali kutangaza kufunga anga ya Tanzania Mei 7, mwaka huu.

 

Hayo yameelezwa na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwelwe, alipozungumza na waandishi wa habari katika ofisi za wizara hiyo zilizopo Mji wa Serikali Mtumba jijini hapa.

“Mtakumbuka kuwa Mei 7, mwaka huu, serikali iliweka zuio kwa ndege za abiria za mashirika ya ndege ya kimataifa kuingia nchini, zuio lililotokana na kuongezeka kwa kuenea kwa mlipuko wa ugonjwa wa homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi vya corona,” alisema Kamwelwe.

 

Zuio kama hili liliwekwa na nchi nyingi duniani,  na lilikuwa ni sehemu ya mkakati wa kudhibiti kuenea kwa homa ya Covid-19 hasa baada ya kubainika usafiri wa anga unachangia kwa kiasi kikubwa kuendelea virusi hivyo.

 

Kamwelwe alisema baada ya tathmini ya mwenendo wa ugonjwa huo nchini iliyotolewa na Rais John Magufuli juzi, imebainisha kuwa udhibiti wa ugonjwa huo kuendelea kuimarika na kuwa wagonjwa wamekuwa wakipungua katika vituo mbalimbali.

 

“Hivyo serikali inatangaza kufungua anga lake rasmi kuanzia leo (jana) na kupitia tangazo hili natamka kuwa ndege zote za kibiashara, misaada, diplomasia, za dharura na ndege maalumu zinaruhusiwa kuruka, kutia na kupita juu ya anga la Tanzania kama ilivyokuwa awali.

“Tangazo hili linafuta tangazo la Mei 7, mwaka huu lililoweka zuio kwa ndege za abiria za mashirika ya kimataifa kuingia nchini,” alieleza Kamwelwe.

Aidha, alisema pamoja na hatua hiyo, serikali itachukua na kuzingatia taratibu zilizowekwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ya Tanzania.

Leave a Comment