KIUNGOmshambuliaji wa Simba, Miraji Athuman ‘Sheva’ amebainisha kuwa kwake hachagui straika wa kucheza naye kati ya Meddie Kagere na John Bocco kutokana na yeyote anayepangwa naye hucheza vizuri.
Sheva amesema kwamba kwake haangalii ni straika gani ambaye anapangwa kucheza naye kwa sababu amekuwa akielewana na kila mchezaji wanayecheza sambamba.
Kiungo huyo mwenye mabao sita, amesema kwamba kwake hamchagulii kocha wake Sven Vandenbroeck mtu wa kumpanga naye sambamba kwa sababu wamekuwa na uelewano mkubwa na straika yeyote ambaye anapangwa naye.
“Kuhusu kucheza na Bocco au Kagere, kwangu yeyote kati yao hakuna tatizo lolote kucheza nao kwa sababu tunafanya vizuri tukiwa uwanjani.
“Sichagui wa kucheza naye, yeyote anayepangwa basi tutashirikiana vizuri kufanya timu ipate matokeo yale mazuri na yatakayowaburudisha mashabiki wetu,” alisema Sheva.