×

Mkapa Asimulia Bibi Yake Kuuawa kwa Tuhuma za Uchawi

KATIKA maisha ya kimaskini kwenye Kijiji cha Lupaso, familia ya hayati Benjamin Mkapa ilikuwa inaonekana kuwa na maisha mazuri.

 

Utofauti wa familia hiyo na wengi kijini hapo ulitokana na uhakika wa kipato alichokuwa akikipata kila mwisho wa mwezi. Hilo halikuwafurahisha wengi na kujenga wivu uliosababisha kutokea kwa shambulio ambalo nusura liangamize familia yao.

 

Hicho ni moja ya visa vya maisha ya hayati rais huyo mstaafu wa awamu ya tatu wa Tanzania ambacho amekihadithia mwenyewe katika kitabu chake cha maisha yake ambacho alikizindua Disemba 2019. Mzee Mkapa alifariki usiku wa kuamkia Ijumaa, Julai 24, 2020, na amezikwa jana Kijijini Lupaso, Masasi mkoani Mtwara.

 

Baba yake, William Matwani,  alikuwa Katekista wa Kanisa Katoliki kijijini hapo pamoja na kufanya kazi ya ualimu, hivyo alikuwa na kipato cha uhakika, kila mwisho wa mwezi, japo kilikuwa kidogo, lakini halikuwa jambo la kawaida katika kipindi hicho cha ukoloni.

 

“Jambo jingine ambalo ni la nadra ni kuwa watoto wote wanne katika familia yetu, pamoja na dada yangu, tulikuwa tumesoma. Hii ilimaanisha kuwa tulikuwa na mustakabali mzuri maishani lakini pia ilitutofautisha na wengine kijini kwetu,” hayati Mkapa anasimulia katika kitabu chake.

‘Tuhuma za Kuzuia Mvua’

Mkapa anasimulia kuwa akiwa na miaka takriban nane ama tisa kulitokea ukame mkali kijijini kwao uliowaacha wengi wakikabiliwa na njaa. Japo kijijini hapo kulikuwa na Wakristo na Waislamu wachache, wanakijiji wengi walikuwa wanaamini katika uchawi na kuamini kuwa kuna mtu ambaye amezuia mvua kunyesha.

 

“Mganga wa kienyeji alitafuta nyumba ya mchawi na kutua kwenye nyumba ya bibi yangu na bibi yangu mkuu. Umati mkubwa wa watu kutoka vijiji kadhaa ulitufuata na kuwaburuza bibi zangu na mama yangu ambao walihojiwa, kupigwa na kuteswa wakishurutishwa kukiri kuwa ni wachawi na wamezuia mvua kunyesha.”

 

Tukio hilo lilitokea wakati baba yake Mkapa akiwa amesafiri kikazi, na mjomba wake Benjamin akiwa ameenda kutafuta kibarua kwenye shamba la katani Lindi. Mkapa na Kaka yake Bernard ambaye alikuwa na miaka 12 walijaribu kuzuia shambulio hilo bila mafanikio.

 

“Nakumbuka kaka yangu alijaribu kuwalinda mama na bibi zangu kutoka kwa kundi la washambuliaji lakini alisukumwa kando na wakubwa,” anaeleza Mkapa: “Ni tukio ambalo lilituathiri wote, nasikia maumivu mpaka leo nikilikumbuka…sitasahau kiluchotokea.”

 

Vurumai hilo liliendelea mpaka Padri Mzungu alipojitosa kuwaokoa wanawake hao watatu kutoka kwenye mikono ya watesi wao. Baadhi ya walioshiriki katika tukio hilo walikamatwa na kufungwa kuanzia miezi 18 mpaka miaka miwili. baada ya Mkuu wa Wilaya kuarifiwa kilichotokea, jambo ambalo lilipunguza makali ya wanakijiji.

 

Bibi Mkuu wa Mkapa alifariki muda mfupi baada ya tukio hilo

“Baada ya muda uadui wa wanakijiji ukatoweka, na licha ya kilichotokea haikuvunja upendo wetu kwa jirani zetu. Tulisalia kijijini hapo. Baba yangu alifuata maandiko yanayosema inakupasa umpende jirani yako.”

 

‘Jina la Ukoo la Mama’

Katika kitabu chake pia anaeleza kuwa jina lake la ukoo, Mkapa, ni la upande wa mama yake Bi Stephania na si baba yake. Mkapa anatoka kwenye kabila la Makua ambao kiasili mtoto ni wa mama, na ubini hupewa na upande wa mama badala ya baba kama ilivyozoeleka katika jamii nyingi.

 

Kabila hilo lipo mpakani baina ya nchi ya Tanzania na Msumbiji, na Mkapa anahadithia kuwa babu yake alivuka Mto Ruvuma kutoka upande wa Msumbiji na kuingia upande wa pili wa Tanzania ya sasa ili kupata ardhi bora ya kulima.

Leave a Comment