ZAIDI ya madaktari 300 wanaofanya kazi katika hospitali za umma katika mji mkuu wa Kenya, Nairobi, wameanza mgomo wakishinikiza malipo bora na kuboreshwa kwa hali zao za kazi ikiwa ni pamoja na vifaa vya kujikinga na maambukizi (PPE).
Nairobi ndiyo mji wenye idadi kubwa ya watu wenye maambukizi ya virusi vya corona nchini humo. Madaktari wanasema kuwa wamekuwa na subira kwa serikali ambayo inahusika na huduma za afya jijini Nairobi.
Mwenyekiti wa madaktari, Thuranira Kaugira, ameandika kwenye akaunti yake ya tweeter kuwa wafanyakazi wa afya wamekuwa maskini vya kutosha. Madaktari wanataka kulipiwa bima kamili ya matibabu na vifaa bora vya kujikinga wanapowashughulikia wagonjwa wa Covid-19.
Hii si mara ya kwanza kwa madaktari wa Kenya kufanya mgomo wakidai malipo na hali bora za kazi. Wahudumu wa afya 700 ni miongoni mwa watu zaidi ya 30,000 waliopata maambukizi ya Covid-19 nchini Kenya. Pia, wahudumu kadhaa wa afya ni miongoni mwa watu waliokufa kutokana na virusi vya corona.




