Aliyekuwa muigizaji wa filamu za Kibongo na mshereheshaji maarufu nchini, Gladys Chiduo maarufu kama Zipompapompa, mwili wake jana jioni ulipumzishwa kwenye nyumba yake ya milele kwenye Makaburi ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam.
Mazishi hayo yalihudhuriwa umati mkubwa wa waombolezaji wakiwemo mastaa wenzake huku washereheshaji na wasanii wa filamu za kibongo wakifurika zaidi.
Katika mazishi hayo watoto wa marehemu, Herry, Fadhili na Dada yao Enzelani waliongeza simanzi kwa waombolezaji wakati wakienda kuweka shada la maua kwenye kaburi la mama yao huku wakionesha huzuni iliyopenya mioyoni mwa waombolezaji.
Katika mazishi hayo upande wa serikali uliwakilishwa na Kaimu Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu Tanzania, Dkt. Kiango Kilonzo aliweka udongo na taji la maua kwenye kaburi la marehemu.
Wengine walioweka taji ni pamoja na msanii wa vichekesho Joti, Pierre Liquid na wengineo.
Zipompapomba enzi za uhai wake alisifika sana kwa ucheshi wake haswa alipokuwa kwenye kazi ya ushereheshaji jambo lililosababisha kuongezeka kwa wateja wake kila kulipokucha huku akihitajika kwenye uigizaji.
Zipompa alipatwa na umauti usiku wa kuamkia Jumatano iliyopita Novemba 10 mwaka huu baada ya kuzidiwa akiwa nyumbani kwake Mbweni jijini Dar na kukimbizwa Hospitali ya Rabininsia iliyopo Tegeta Dar.












