×

Ratiba Kamili Rais Samia Atakavyohutubia Bunge kwa Mara ya Kwanza

Leo Alhamisi Aprili 22, 2021 kuanzia saa 10 jioni Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan atalihutubia Bunge kwa mara ya kwanza tangu alipoapishwa kuwa kiongozi mkuu wa nchi Machi 19, 2021.

 

 

Kwa mujibu wa ratiba ya Bunge iliyotolewa leo inaonyesha kuwa hotuba ya Rais itaanza saa 10:10 jioni lakini asubuhi kuanzia saa 3:00 hadi saa 5:00 kutakuwa na kikao cha kawaida cha Bunge.

 

 

Saa 5 asubuhi hadi saa 8 mchana ndani ya ukumbi wa Bunge kutakuwa na shughuli za kiutawala zitakazosimamiwa na katibu wa Bunge au mkuu wa itifaki bungeni na kuanzia saa 8 mchana hadi saa 9 alasiri utakuwa ni muda wa wabunge na wageni waalikwa kuingia ukumbini na maeneo maalum ya wageni.

 

 

Saa 9:15 hadi saa 9:50 alasiri utakuwa ni muda wa viongozi mashuhuri kuingia bungeni ambao ni Jaji Mkuu wa Tanzania, Jaji Mkuu wa Zanzibar, Makamu wa Kwanza wa Rais – Zanzibar, Makamu wa Pili wa Rais – Zanzibar, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

 

 

Saa 9:55 alasiri Spika wa Bunge, Job Ndugai ataingia ndani ya ukumbi wa Bunge na mara watakapowasili wimbo wa Taifa na Wimbo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki utaimbwa kisha Spika atatoa maelezo kwa dakika tano hadi saa 10:10 jioni.

 

 

 

Baada ya hapo Rais Samia atatoa hutuba yake kwa muda ambao haujatajwa na akimaliza mbunge wa Kahama Mjini (CCM), Jumanne Kishimba atatoa neno la shukrani kwa niaba ya Bunge kisha Spika atafanya utambulisho wa viongozi na wageni waalikwa.

 

 

 

Baada ya hatua hiyo Ndugai na Samia watatoka ndani ya ukumbi wa Bunge na kuelekea kwenye chumba maalum wakifuatiwa na viongozi mashuhuri kisha Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa atatoka ukumbini kuelekea eneo la picha kisha wabunge nao watafuata kuelekea eneo hilo.

Leave a Comment