The House of Favourite Newspapers

Kisa Manyama, Simba Yarudi Rasmi Kwa Luhende

0

BAADA ya kugonga mwamba kwenye usajili wa beki wa Ruvu Shooting, Charles Manyama ambaye ametua Azam FC, Kocha wa Simba, Mfaransa, Didier Gomes Da Rosa, ameusisitiza uongozi wa timu hiyo kuhakikisha unamsajili beki mwingine wa kushoto, na sasa wamerudi rasmi kumuwania David Luhende.

 

Kwa takriban mwezi mmoja, uongozi wa Simba ulikuwa kwenye harakati za kutaka kumsainisha Manyama huku ukimtengea kitita kinono cha milioni 50, lakini mipango yao iligonga mwamba baada ya Azam FC kumtangaza mapema wiki iliyopita Chanzo chetu kutoka ndani ya Simba, kimelieleza Championi Jumatano kwamba, uongozi huo ulishindwa kumalizana na Manyama mapema kwa kuwa ulikuwa ukisubiria ruhusa ya kocha wao Gomes ambaye alikuwa kwao Ufaransa, na sasa amerejea na kuwataka watafute mwingine.

“Ukweli uliopo ni kwamba, sisi hatukushindwa kumsajili Manyama eti kwa sababu Azam walituzidi akili, ila tulikuwa tunashindwa kumalizana naye kufuatia kutokuwa na jibu la moja kwa moja kutoka kwa kocha ambaye alikuwa amesafiri, na hata siku ya mwisho hatukumpata kocha jambo ambalo Azam walilitumia vyema kutupiku.

 

Hatuna shaka sana na hilo nadhani muda wowote sasa karata yetu itaangukia kwa Luhunde ambaye kimsingi naye tulishafanya mazungumzo ya awali zaidi tunaangalia namna ya kumalizana na waajiri wake Kagera Sugar,” kilisema chanzo hicho.

 

Championi lilizungumza na Mkuu wa Maudhui wa Simba, Ally Shatry ‘Bob Chico’, ili kujua juu ya taarifa hizo, ambapo alisema: “Kwa sasa mimi sina maelezo kamili juu ya usajili, hivyo ni vyema ukamtafuta kocha Gomes maana yeye ndiye mwenye kujua nani anamtaka au yupi hamtaki.”

STORI: MUSA MATEJA,Dar es Salaam

Leave A Reply