
MKUU wa Upelelezi Wilaya ya Kipolisi ya Kariakoo, Dkt. Ezekiel Kyogo amewaongoza viongozi wa ulinzi shirikishi na waendesha bodaboda wa eneo hilo katika mafunzo maalum ya kudhibiti na kupambana na uhalifu. Dkt. Kyogo alitoa mafunzo kwa wadau hao yaliyofanyika Baa ya Wazee iliyopo Amana jijini Dar na kuwaeleza madereva wa bodaboda jinsi ya kuwatambua wahalifu wakiwemo majambazi wanaotaka kuwaua na kuwapora pikipiki zao.

Afande Kyogo amesema katika maisha maendeleo hayawezi kuja bila usalama kwa maana usalama ndiyo kila kitu. Akizungumza kwenye mkutano huo amefafanua la mkutano huo ni kuzungumza na bodaboda hao kwa kuwa ndiyo wadau wakubwa wa masuala ya usalama.

“Bodaboda nyie ni wadau wakubwa sana wa usalama kwakuwa ndiyo mnaowabeba watu mbalimbali wakiwemo hao wahalifu hivyo mkiamua kuwa wazalendo mtautokomeza huo uhalifu. “Unakuta bodaboda wasio wazalendo ndiyo wanaowabeba vishandu ‘wapora simu’ ambao wakishapora bodaboda ndiyo wanaowakimbiza.

Wengine ndiyo wanaotumika kubeba mizingo ya wizi au haramu na kwakuwa wengine hawana uzalendo hawatoi ushirikiano kwa polisi au ulinzi shirikishi.
Katika mafunzo hayo afande huyo aliwataka bodaboda hao kutambua nafasi zao katika suala la ulinzi na kuwaambia kuwa wao ndiyo wanaotegemewa sana katika ushirikiano wa kiusalama.
Bodaboda hao walifundishwa kuwakataa abiria wanaoomba kubebwa mshakaki haswa nyakati za usiku ili kuepusha vitendo vya kuweza kubadilikiwa na kuzidiwa nguvu na wahalifu hao kwakuwa ni rahisi kukuzidi nguvu. Baada ya mafunzo hayo Afisa Mtendaji Kata ya Ilala, Majura Mutalemwa aliwaasa waendesha bodaboda hao viongozi wa ulinzi shirikishi kuyazingatia mafunzo yaliyotolewa na Dkt. Kyogo kwa maendeleo ya Ilala, Kariakoo na kwingineko kwa ujumla.

Mutalemwa alimsifu kamanda huyo kwa mafunzo hayo na kuwaomba walioshiriki wote kuyazingatia. Nao baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo wakielezea furaha yao baada ya kufundishwa uzalendo wa kuipenda nchi yao na kujilinda wao wenzao na mali zao na kusema wanaenda kuwa mabalozi wa kusambaza imani ya kizalendo kwa wenzao. Mkuu wa Ulinzi Shirikishi eneo la Machinga Complex, Wilfred William kwa upande wake alieleza jinsi hali ya usalama ilivyorejea eneo hilo tangu walipoanza kulishwa imani ya kizalendo na Dkt Ezekiel miongoni mwao na kutakiwa kushirikiana na jeshi la polisi kwa kupewa njia ya mawasiliano ya haraka mara waonapo dalili zisizo nzuri. HABARI/PICHA NA RICHARD BUKOS NA ISSA MNALLY /GPL