
Muigizaji nyota wa tamthilia maarufu Duniani ya ‘Squid Game’ O Yeong-su amefanikiwa kushinda tuzo ya kwanza ya Glolden Globe kama muigizaji bora msaidizi kwenye tamthilia hiyo.
Muigizaji huyo wa Korea Kusini mwenye umri wa miaka 77 aliyeigiza kama Oh II-nam, anayejulikana pia kama The Host au Player 00 katika mfululizo wa tamthilia hiyo.
Huu umekuwa uteuzi wake wa kwanza kwenye tuzo za Golden Globe na kufanikiwa kushinda, na pia ndiye mwigizaji wa kwanza wa Korea katika historia ya Golden Globes kushinda tuzo hizo kubwa Duniani.
Haikuwa rahisi kwa mzee O Yeong-su kujinyakulia tuzo hiyo, alikabiliana na ushindani mkali kutoka kwa mastaa wengine kadhaa na kufanikiwa kuwapiga chini wakali kama Billy Crudup (The Morning Show), Kieran Culkin (Succession), Mark Duplass (The Morning Show) pamoja na Brett Goldstein (Ted Lasso).
O Yeong-su alianza kazi yake jukwaani na ameonekana katika maonesho takribani 200 ya maigizo, baadaye aliamua kuhamia kwenye maonesho ya televisheni na kwenye kumbi za michezo katika miaka ya sabini bila kufanikiwa kwa kiwango kikubwa sawa na hivi sasa.
Ambapo amejizolea umaarufu mkubwa kote Duniani kupitia tamthilia ‘Squid Game, ambayo ni tamthilia iliyoongoza kwa kutazamwa zaidi kupitia mtandao wa Netflix katika nchi takribani 94, na kaya milioni 142 zinaaminika kuitazama.
Mnamo Oktoba 2021, O Yeong-su kwenye moja ya mahojiano alidokeza kidogo kuhusu mafanikio aliyoyapata na kusema, “Ninahisi kama ninaelea hewani.”
Akibainisha kiwango cha furaha aliyonayo juu hali halisi ya maisha yake baada ya tamthilia hiyo kumtoa sehemu moja hadi nyingine kimafanikio.