
KIUNGO mshambuliaji wa klabu ya Brentford ya nchini Uingereza Christian Eriksen amekubali kujiunga na miamba ya soka nchini Uingereza klabu ya Manchester United kwa mkataba wa miaka 3.

Eriksen (30) aliyewahi kuvichezea vilabu mbalimbali barani Ulaya kama vile Ajax Amsterdam, Totenham Hotspurs, Inter Milan pamoja na Brentford ameonesha nia hiyo ikiwa ni sehemu ya ndoto yake ya kufanya kazi na kocha mpya wa sasa wa Manchester United raia wa Uholanzi Erik Ten Hag.

Msimu uliopita kiungo huyo alilazimika kucheza kwa mkopo katika klabu ya Brentford baada kupona kutokana na shambulio la moyo alilolipata katika mashindano ya Euro 2020 yaliyofanyika mwaka jana.
Nyota huyo anayeiwakilisha Timu ya Taifa ya Denmark amekuwa katika kiwango kizuri na kuiwezesha klabu ya Brenford kubaki Ligi Kuu ya Uingereza.