
Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) limefanya mashambulizi makubwa ya anga dhidi ya ngome za waasi wa Houthi nchini Yemen usiku wa kuamkia Jumatatu, saa chache baada ya kutoa agizo la dharura la kuhama kwa raia katika maeneo matatu muhimu yanayodhibitiwa na Houthi. Saa chache baadaye, Houthi walirusha makombora mawili ya masafa marefu dhidi ya Israel, na kusababisha ving’ora vya tahadhari kuunguruma katika makazi kadhaa ya Ukingo wa Magharibi.
Kwa mujibu wa taarifa rasmi ya IDF, mashambulizi hayo yalitekelezwa na ndege 20 za kivita za Israeli na kulenga maeneo kadhaa muhimu ya kijeshi ya Houthi ikiwemo bandari za Hodeidah, Ras Isa na Salif, pamoja na kituo cha umeme cha Ras Khatib.

Mashambulizi hayo pia yaliilenga meli ya Galaxy Leader ambayo ilitekwa na Houthi tangu Novemba 2023 na kutumiwa kwa ufuatiliaji wa baharini na kupanga operesheni. Meli hiyo ilikuwa na wafanyakazi 25 kutoka Ufilipino, Bulgaria, Romania, Ukraine na Mexico ambao walikuwa mateka tangu Januari 2025.