
MTOTO wa kike mwenye umri wa miaka 13, mkazi wa eneo la Isakalilo katika Mtaa wa Njiapanda, Manispaa ya Iringa, ambaye alikuwa mwanafunzi wa darasa la saba katika Shule ya Msingi Zizi, amefariki dunia baada ya kudaiwa kufanyiwa ukatili wa kingono.
Kwa mujibu wa majirani na ndugu wa familia waliozungumza na Global TV, mwili wa mtoto huyo uligunduliwa majira ya asubuhi nje ya nyumba yao, baada ya familia na majirani kuanza kumtafuta kufuatia kutomuona tangu usiku wa kuamkia siku hiyo.
Tukio hilo limesababisha taharuki na huzuni kubwa kwa wakazi wa eneo hilo, huku wengi wakitaka hatua kali zichukuliwe dhidi ya wahusika.
Akizungumzia tukio hilo, Mwenyekiti wa Mtaa wa Njiapanda, Maisha Modestus, amesema ni tukio la kusikitisha na la kutisha kwa jamii, na kwamba tayari taarifa zimetolewa kwa vyombo vya dola ili uchunguzi wa kina ufanyike.
Ameongeza kuwa uongozi wa mtaa unaendelea kushirikiana na mamlaka za usalama ili kubaini chanzo cha tukio hilo na kuwabaini wahusika ili wachukuliwe hatua za kisheria.