×

Wakili wa Besigye Ashtakiwa kwa Kosa la Uhaini Uganda

Meya wa zamani wa Kampala na wakili wa kiongozi wa upinzani nchini Uganda, Kizza Besigye, Erias Lukwago, amefikishwa mahakamani na kushtakiwa kwa kosa linalohusiana na uhaini siku chache baada ya kukamatwa nyumbani kwake.

Lukwago alifikishwa mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkuu jijini Kampala akiwa katika hali iliyodaiwa kuonekana dhaifu, kwa mujibu wa taarifa za vyombo vya habari vya ndani. Hata hivyo, alikanusha mashtaka yote yanayomkabili na kuamriwa kurejeshwa rumande hadi kesi yake itakaposikilizwa wiki ijayo.

Kukamatwa kwa mwanasheria huyo Jumatatu ya wiki hii kumezua mjadala mkubwa nchini Uganda, hasa baada ya Mkuu wa Majeshi ya Uganda, Jenerali Muhoozi Kainerugaba, ambaye pia ni mwana wa Rais Yoweri Museveni, kuchapisha ujumbe kwenye mitandao ya kijamii akizungumzia tukio hilo.

Kiongozi wa upinzani Robert Kyagulanyi, maarufu kama Bobi Wine, amedai kuwa Lukwago alikamatwa kwa maelekezo ya Kainerugaba wakati akijiandaa kuwasilisha hati ya wito wa mahakama dhidi yake.

Kupitia ukurasa wake wa mtandao wa X, Bobi Wine alikosoa tukio hilo na kutoa wito wa kupingwa kwa kile alichokiita kuporomoka kwa utawala wa sheria nchini humo.

Wakati huo huo, familia ya Lukwago ilifungua shauri mahakamani ikitaka vyombo vya usalama vifichue alikokuwa akishikiliwa baada ya madai ya kutoweka kwa muda tangu alipokamatwa. Familia hiyo pia imeendelea kudai kuwa Kainerugaba alihusika moja kwa moja na kukamatwa kwake kutokana na machapisho yake kwenye mitandao ya kijamii.

Kesi hiyo imeongeza wasiwasi kuhusu hali ya kisiasa nchini Uganda huku kukiwa na ongezeko la malalamiko kutoka kwa wanasiasa wa upinzani kuhusu kile wanachodai kuwa ni ukandamizaji wa sauti zinazopinga Serikali.

Leave a Comment