×

Congo DR Yapiga Marufuku Mikusanyiko Kisa Ebola

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imetangaza marufuku ya mikusanyiko ya umma katika majimbo manne yaliyotajwa kuwa katika hatari kubwa ya maambukizi ya Ebola, kwa mujibu wa vyombo vya habari vya nchini humo.

Waziri wa Mambo ya Ndani, Jacquemain Shabani, amesema hatua hiyo inahusu majimbo ya Kinshasa, Tshopo, Bas Uele na Haut Uele, na inajumuisha kusitishwa kwa mikutano, maandamano na mikusanyiko mingine ya watu wengi hadi itakapotangazwa vinginevyo.

Maafisa wa serikali wanasema hatua hiyo inalenga kuimarisha udhibiti wa Ebola, wakionya kwamba harakati kubwa za watu ndani na karibu na maeneo yaliyoathirika zinaweza kuongeza hatari ya kuenea kwa ugonjwa huo.

Takwimu za serikali zinaonyesha kuwa hadi sasa kuna visa 1,203 vilivyothibitishwa vya Ebola na vifo 321, huku kitovu cha mlipuko huo kikiwa katika jimbo la Ituri.

Majimbo jirani ya Kivu Kaskazini na Kivu Kusini pia yamewekwa chini ya uangalizi maalumu.

Leave a Comment