×

Ufaransa Yaifumua Sweden 3-0, Mbappe Ang’ara, Yatinga 16 Bora Kombe la Dunia

EAST RUTHERFORD, New Jersey: Nahodha wa Ufaransa, Kylian Mbappe, aliendelea kuonyesha ubora wake katika Kombe la Dunia 2026 baada ya kufunga mabao mawili na kuiongoza timu yake kuichapa Sweden mabao 3-0 katika hatua ya 16 Bora.

Mbappe alifunga mabao yake ya 17 na 18 katika historia ya Kombe la Dunia, na sasa amebakiwa na bao moja tu kumfikia Lionel Messi kwenye orodha ya wafungaji bora wa muda wote wa michuano hiyo.

Aidha, mabao hayo yamemfikisha sita kwenye Kombe la Dunia la mwaka huu, akilingana na Messi katika mbio za kuwania Kiatu cha Dhahabu.

Bradley Barcola alifunga bao la tatu la Ufaransa kipindi cha pili, huku Michael Olize akitoa pasi mbili za mabao katika ushindi huo uliowafanya mabingwa hao wa dunia mara mbili kuendelea na rekodi yao bora ya kushinda mechi zote nne walizocheza, wakiwa wamefunga mabao 13 na kuruhusu mawili pekee.

Kocha Didier Deschamps sasa ataipeleka Ufaransa kwenye robo fainali ambapo itakutana na Paraguay mjini Philadelphia siku ya Jumamosi. Paraguay ilitinga hatua hiyo baada ya kuiondoa Ujerumani kwa mikwaju ya penalti kufuatia sare ya 1-1.

Kwa upande wa Sweden, safari yao imefikia tamati baada ya kampeni yenye matokeo yaliyobadilika mara kwa mara. Walianza kwa kuifunga Tunisia 5-1, wakapokea kipigo cha mabao 5-1 kutoka Uholanzi, kabla ya kutoka sare ya 1-1 dhidi ya Japan na kufuzu hatua ya mtoano. Hii ilikuwa mara yao ya kwanza kuvuka hatua ya makundi kwenye mashindano makubwa tangu Euro 2020, huku wakikosa kufuzu Kombe la Dunia 2022 na Euro 2024.

Ufaransa ilitawala mchezo tangu mwanzo, huku Mbappe na Olize wakigonga mwamba wa lango kabla ya Jacob Widell Zetterstrom kuokoa hatari kadhaa.

Baada ya nafasi hizo kupotea, Mbappe aliifungia Ufaransa bao la kwanza dakika ya 45. Olize na Ousmane Dembele walicheza kona ya haraka iliyomkuta Mbappe upande wa kushoto wa eneo la hatari, kabla ya mshambuliaji huyo kumpita Viktor Gyokeres na kupiga shuti kali lililojaa wavuni.

Dakika nane baada ya mapumziko, Barcola aliandika bao la pili akimalizia pasi safi ya Olize kwenye shambulizi la kushtukiza.

Mbappe alihitimisha ushindi huo dakika ya 74 baada ya kupokea pasi nyingine ya Olize na kufunga kwa ustadi, akifanana na namna alivyofunga bao lake la kwanza.

Dakika 11 baadaye, Deschamps alimtoa Mbappe kupumzika huku akishangiliwa kwa makofi na mashabiki waliofurika katika Uwanja wa New York New Jersey Stadium.

Leave a Comment