×

Ufaransa Waweka Kifua Mbele, Waapa Kuizuia Hispania Kutinga Fainali Kombe la Dunia 2026

WALTHAM, Marekani: Beki wa timu ya taifa ya Ufaransa, Ibrahima Konate, amesema kikosi chao hakina hofu ya kuikabili Hispania katika mchezo wa nusu fainali ya Kombe la Dunia 2026, lakini kinaiheshimu kutokana na ubora mkubwa ilioonyesha katika mashindano hayo.

Akizungumza na waandishi wa habari Jumapili, Konate alisema hakuna sababu ya kuogopa mpinzani yeyote katika hatua hii ya mashindano, huku akisisitiza kuwa Ufaransa itajiandaa kikamilifu ili kuhakikisha inapata ushindi.

“Huwezi kumuogopa mpinzani yeyote. Tutajiandaa vizuri kadri tuwezavyo na tunatumaini matokeo yatakuwa upande wetu,” alisema Konate.

Hispania imefika hatua ya nusu fainali ikiwa imeruhusu bao moja pekee katika mashindano yote na inaendelea kuwinda taji lake la pili la Kombe la Dunia.

Konate aliisifu Hispania kwa kuwa na kikosi chenye ubora mkubwa wa wachezaji binafsi, akisema Ufaransa haitajikita kumzuia nyota mmoja pekee, licha ya kiwango bora kinachoonyeshwa na Lamine Yamal.

“Hispania ni timu ya kipekee yenye wachezaji wengi wenye uwezo mkubwa. Hatutakuwa tunamfikiria Lamine Yamal pekee, ingawa ni mchezaji bora,” aliongeza.

Ufaransa, mabingwa wa Kombe la Dunia mwaka 2018 na washindi wa pili mwaka 2022, wanafahamu vyema nguvu ya Hispania baada ya kufungwa nao katika nusu fainali ya Euro 2024 na pia kwenye Nations League mwaka uliopita.

Iwapo Ufaransa itafanikiwa kuiondoa Hispania na kutinga fainali itakayochezwa Julai 19 jijini New York, itakuwa imefika fainali yake ya tano ya Kombe la Dunia katika historia, jambo litakalozidi kuithibitisha kuwa miongoni mwa mataifa makubwa zaidi katika soka la dunia.

Leave a Comment