The House of Favourite Newspapers

Mwinyi Zahera: Lwandamina Hanizuii

KOCHA Mkuu wa Yanga, Mwinyi Zahera ametamba kwamba licha ya kwamba anakutana na kocha ambaye aliwahi kuinoa Yanga, George Lwandamina, lakini hana hofu hata kidogo kwani mpinzani wake hazijui mbinu zake.

 

Zahera akiwa na kikosi cha Yanga, atakutana na Lwandamina anayeinoa Zesco United katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya kwanza ambapo mechi ya kwanza itapigwa Septemba 14, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar kabla ya kwenda kurudiana nchini Zambia.

 

Zahera raia wa DR Congo ameliambia Championi Jumatatu, kuwa kwake hana hofu hata chembe ya kukutana na Lwandamina ambaye anajua mazingira ya klabu hiyo kwani hajui anatumia mfumo pamoja na mbinu gani.

 

“Kweli kabisa nakutana na mtu ambaye amewahi kufundisha hapa, lakini ukweli ni kuwa mimi hanijui hata kidogo.

 

“Yeye amepita hapa na anajua mazingira mazima ya Yanga lakini nachosema hilo halinipi shaka kwani mimi ni mtu mwingine na ninatumia mifumo na mbinu nyingine tofauti na zile ambazo alikuwa akifundisha alipokuwepo hapa.

 

“Hatuwezi kuwaogopa Zesco hata kwa namna moja na badala yake tunajipanga kukamilisha kile ambacho tumejipangia kukifanya kwenye hatua hii. Kitu kimoja ambacho nataka kusema ni kuwa mashabiki waje kwa wingi katika mchezo huo kwa sababu wao watatupa nguvu zaidi ya kukamilisha malengo yetu,” alisema Zahera.

SAID ALLY, Dar es Salaam

Comments are closed.