Pablo Awasoma Ruvu Shooting Kwa Video
HUKU wakijipanga na mchezo wa leo Ijumaa dhidi ya Ruvu Shooting kocha mkuu wa Simba, Pablo Franco amefichua kuwa ameisoma timu hiyo kupitia video walipocheza na Yanga.
Simba walio katika nafasi ya pili kwenye msimamo, leo Ijumaa watakuwa wageni wa Ruvu Shooting katika mchezo wa ligi kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.
Baada ya mchezo wa leo dhidi ya Ruvu Shooting, Simba watasaliwa na mchezo mmoja tu dhidi ya Geita Gold utakaopigwa Desemba 1, kabla ya kuwavaa Yanga Desemba 11, mwaka huu.
Akizungumza na Championi Ijumaa, kocha Pablo alisema: “Tunaenda kucheza mchezo mgumu dhidi ya Ruvu Shooting, nimepata nafasi ya kuwaona Ruvu Shooting kupitia kanda za video za mchezo wao dhidi ya Yanga ambapo walianza kufunga bao la kuongoza na inawezekana kama wasingepata kadi nyekundu basi Yanga wasingeweza kushinda.
“Nimewatazama Yanga pia kupitia mchezo ule na michezo yao mingine na najua ushindani nitakaokutana nao, sina presha na hilo na nafurahia changamoto hii mpya.”
STORI: JOEL THOMAS | CHAMPIONI IJUMAA