The House of Favourite Newspapers

Zahera Ashusha Winga Matata Mnyarwanda

IMEFAHAMIKA kuwa winga hatari wa kulia na kushoto anayekipiga Klabu ya Mukura Victory Sports ya Rwanda, Patrick Sibomana, usiku wa kuamkia jana alipanda ndege ya RwandAir na kutua nchini kwa ajili ya kufanya mazungumzo na Yanga.

 

Kocha Mkuu wa Yanga Mkongomani, Mwinyi Zahera aliwahi kuliambia Gazeti la Championi kuwa yupo kwenye mazungumzo na baadhi ya wachezaji sita wa kimataifa watakaokuja kuichezea timu hiyo kutoka Rwanda, Nigeria, Ivory Coast na Guinea.

 

Hiyo yote ni katika kukiimarisha kikosi chake kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Bara ambao Yanga imepania kuuchukua ubingwa.

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumatatu, winga huyo anakuja kwa ajili ya mazungumzo kabla ya kupewa mkataba wa kuichezea timu hiyo.

“Muda mrefu Yanga walikuwa wanamuwania winga huyo tangu msimu uliopita, baada ya kushindikana kukamilisha usajili wake.

“Lakini msimu huu wamepanga kumsajili katika kukamilisha ripoti ya kocha aliyoitoa ya kukamilisha usajili wa kila mchezaji anayemuhitaji katika kuelekea msimu ujao,” alisema mtoa taarifa huyo.

 

Makamu mwenyekiti wa timu hiyo, Frederick Mwakalebela, alipotafutwa kuzungumzia hilo, alisema: “Siwezi kukubali au kukataa ujio wa winga huyo, ukweli wapo wachezaji wengi wanaotarajiwa kutua nchini kwa ajili ya kusajiliwa, hivyo tusubirie suala hilo kama likikamilika tutaweza wazi.”

 

Jana jioni Championi lilimshuhudia winga huyo akiwa hoteli moja jijini Dar na viongozi wa Yanga akiwemo Mwakalebela na Samuel Lukumay wakifanya mazungumzo ya kumpa mkataba ambao unaaminika ni wa miaka miwili.

MUSA MATEJA, Dar es Salaam

Comments are closed.