×

Freeman Mbowe: Polisi Wanaogopa Kutoa Brass Band, Wananiambia Niongee na IGP (Video)

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.

NI simanzi. Ndivyo unaweza kusema baada ya maelfu ya wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro, hasa mji wa Moshi na miji ya jirani kufurika katika ibada ya kumuaga aliyekuwa Mbunge wa Moshi Mjini, marehemu Philemon Ndesamburo (82).

Tukio hilo la kuaga mwili wa Ndesamburo maarufu kama Ndesa Pesa, lilifanyika jana mjini Moshi na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali, huku maduka na shughuli za kijamii zikisimama kutwa.

Akizungumza uwanjani hapo, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema: “Sina hakika nizungumze nini kwani jambo hili kwetu ni gumu sana kulizoea, utahitaji muda mwingi sana kumwelezea Ndesamburo ni nani, unaweza kumaliza hata siku nzima au wiki nzima, ni baraka tosha huyu mzee si wa kawaida.

“Inafika mahali tunapita hakuna mahali pa kulala kwa sababu wote wenye nyumba za kulala ni watu ambao pengine ni wa chama kingine, chama kile au pengine ni watu wao wanatunyima mahali pa kulala, tumelala kwenye magari na Ndesamburo mara nyingi kwa kunyimwa mahali pa kupumzika tukiwa katika harakati za kisiasa,” alisema.

WANYIMWA BENDI YA POLISI

Akizungumzia magumu waliyokutana nayo katika msiba huo, Mbowe alisema ni pamoja na kunyimwa uwanja na bendi ya polisi.

“Kwanza tuliamini kwa tukio hili la kihistoria ni vema mzee wetu tungemsindikiza kwa ‘Brass Band ya Polisi’, tukaenda Chuo cha Polisi Moshi ambacho Mzee Ndesamburo amewafanyia mambo mbalimbali.

“Brass Band hiyo hukodishwa kwa Sh 300,000 na kama wafiwa tayari tulishajiandaa kulipia gharama hizo.

“Wanaogopa kutoa Brass Band, wananiambia niongee na IGP, yaani Mbowe nimpigie IGP simu kumuomba Brass Band, mimi?

“Band hii hukodishwa kwenye Send off za maharusi eti leo polisi wanaogopa hata kufanya kazi kwa sababu hawajui bwana mkubwa atafurahi ama atakasirika.

“Tukahitaji kiwanja tukiamini kwamba Majengo si kwamba hapakuwa panafaa bali tuliamini historia ya Moshi, Uwanja wa Mashujaa kama unavyoitwa unastahili kuwa uwanja wa kumuaga Mzee Ndesamburo, polisi wameweka vigingi,” alisema.

Leave a Comment