
ILE droo ndogo ya tano ya Bahati Nasibu ya Shinda Nyumba Awamu ya Pili itachezeshwa Alhamisi hii katika viwanja vya wazi vya Las Vegas, vilivyopo mkabala na Soko Kuu la Mabibo maarufu kama Soko la Ndizi.

Ofisa Masoko wa Global Publishers, inayoendesha bahati nasibu hiyo kubwa kabisa kuwahi kutokea nchini, Yohana Mkanda alisema jana kuwa kila kitu sasa kimekamilika na kilichobakia ni kwa wasomaji wa magazeti ya Ijumaa, Championi, Uwazi, Risasi, Ijumaa Wikienda na Amani, kujitokeza kwa wingi kushuhudia tukio hilo.

“Ipo faida kubwa kwa wasomaji kushiriki tukio hili la uchezeshaji wa droo yetu ndogo ya tano, kwa sababu licha ya kuweza kubahatika kupata ushindi kwa kupitia kuponi ambazo tayari walishajaza hapo awali, lakini pia eneo la tukio, kuna zawadi nyingi za sapraizi zitatolewa, kwa hiyo ni muhimu kuwepo ili waweze kujiongezea nafasi ya ushindi,” alisema Mkanda.

Droo hiyo ya tano itafanyika ikiwa ni mwendelezo ya droo hizo kuelekea ile kubwa kabisa ambayo mshindi atakabidhiwa zawadi ya nyumba yenye thamani ya mamilioni, ikiwa ni mara ya pili kwa Global Publishers kufanya hivyo, kwani awali Nelly Mwangosi, mama mjasiriamali kutoka Iringa, alijishindia nyumba iliyojengwa maeneo ya Salasala, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.

Katika droo ndogo nne ambazo zimeshafanyika hadi sasa katika Viwanja vya Dar Live, CCM Mwinjuma Mwananyamala na Manzese Bakhresa, jijini Dar es Salaam, zawadi mbalimbali zimeshatolewa kwa washindi zaidi ya 20 ambazo ni pamoja na pikipiki, seti ya televisheni kubwa za kisasa, simu za mikononi za kisasa, seti za vyombo vya nyumbani na ving’amuzi.

Kuhusu droo hiyo ya tano, Ofisa Masoko Mkanda alisema, kama ilivyo ada, zawadi zitatolewa ikiwemo televisheni kubwa, vyombo vya nyumbani na ving’amuzi -na kwamba hiyo yote inatokana na udhamini wa Premier Bet, Tecno Mobile na Kampuni ya Ving’amuzi ya Ting ambao kwa pamoja wamejitokeza kuunga mkono juhudi za Global Publishers kubadili maisha ya watu kupitia Bahati Nasibu ya Shinda Nyumba.
Na Mwandishi Wetu