
Mabao matatu ya Lionel Messi yamekuwa na msada mkubwa katika kuiwezesha Barcelona kubeba ubingwa wa Ligi Kuu ya Hispania ‘LA Liga’ baada ya timu hiyo kuifumua Deportivo mabao 4-2.

Kocha wa Barcelona, Ernesto Valverde alikuwa na furaha baada ya kuishuhudia timu yake ikipata ushindi huo na kufikisha pointi 86 licha ya kuwa upinzani ulikuwa mgumu.

Philippe Coutinho ndiye aliyeanza kufunga bao kisha Messi akafunga la pili, baada ya hapo straika wa zamani wa Arsenal, Lucas Perez akafanikiwa kupata bao la kwanza kwa Deportivo.

Kiungo Emre Colak akaiwezesha Deportivo kusawazisha na matokeo kuwa 2-2, hivyo ikabidi nguvu iongezeke na Messi kufunga mawili dakika za mwisho.

Matokeo hayo yamewpa Barcelona ubingwa wa 25 katika La Liga ikiwa imesalia michezo minne ambapo hawajapoteza mchezo hata mmoja katika ligi hiyo.

Wiki ijayo Barcelona itakipiga dhidi ya Real Madrid katika ligi hiyo.








