
BAADA ya kupita wiki moja tangu siku ya kuzaliwa kwake (Septemba 23), Zari ‘The Bosslady’, mama watoto wa mwanamuziki wa Bongo, Diamond Platnumz, alirejea na kuiadhimisha siku hiyo nyumbani kwao, Uganda katika jiji la Kampala.
Hii ni baada ya Zari kupata misukosuko kadhaa katika uwanja wa ndege wa Heathrow, London, kuhusiana na masuala ya uhamiaji ambako alikaa kwa saa 16 akihojiana na maofisa wa uhamiaji, hivyo kuchelewa kuungana na mashabiki na marafiki zake waliokuwa wamefika uwanjani kumpokea na kufurahi nao katika siku hiyo.
Misukosuko hiyo ilisababisha kudorora kwa maadhimisho ya siku hiyo ambapo alitimiza miaka 38.

Hata hivyo, pamoja na vituko hivyo, alirejea nyumbani Uganda na kusherehekea siku hiyo akiwa na marafiki na ndugu kadhaa wachache ambapo watu maarufu walikuwa ni pamoja na Captain Mike Mukula, dada wa Zari, Aly Alibhai na mkewe, Sylvia Wilson Namutebi.