
POLISI mkoani Njombe linamshikilia mwanamke aliyefahamika kwa jina la Apronia Mwinuka (35) mkazi wa mtaa wa Kikula kata ya Makambako mkoani Njombe kwa tuhuma za kumpiga na kumsababishia kifo Elina Mwinuka (18) kwa kosa la kuchelewa kurudi nyumbani.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Njombe, Hamis Issa, amesema uchunguzi umebaini binti huyo amefariki kutokana na kipigo alichokipata huku ikidaiwa alichelewa kurudi nyumbani kutokana na kupitia kwa mpenzi wake.
“Alichokifanya shangazi ni kutoa adhabu ambapo aliampa kipigo binti huyo akidai alipitia kwa mpenzi wake na kile kipigo kilisababisha binti akafariki dunia wakati akipelekwa kupata matibabu,” alisema Issa.
Mume wa Apronia, Thadei Mhongole, alisema tukio hilo limetokea wakati yeye akiwa kwenye shughuli za utafutaji na aliporudi alikuta binti huyo akiwa amezimia baada ya kupigwa na shanganzi yake.
“Ni mtoto wa kaka’angu kwa kweli kuondokewa na huyu ndugu yangu ninasikitika sana, wito wangu hasa kwa akina mama wawe na kiasi katika kuwaonya watoto,” alisema Mhongole.
Baadhi ya majirani wa familia hiyo wamesema kuwa mwanamke huyo amekuwa na tabia ya kuwaadhibu watoto mara kwa mara.
“Ni kawaida yake kuwaadhibu hata watoto wake mara kwa mara hata wakipoteza mkoba sasa adhabu ya juzi ikawa imezidi kipimo ikampekea mtoto kukata roho kabisa. Tulipokagua kwenye nyumba yao tulikuta kuna njiti za mianzi ambazo alikuwa anamtandikia na vipande viwili vimebanduka kabisa,” alisema mmoja wa majirani.
Kenneth Solomon Kibiki, mwenyekiti wa serikali ya mtaa wa Kipagamo kata ya Makambako, amekemea vitendo hivyo na kusema:
“Tukio hili linatuhuzunisha sana viongozi na tunakemea lisijirudie kwa sababu adhabu zinapitiliza mpaka tunapunguza nguvu kazi ya taifa,” alisema.