MAKUMI ya watu waliokuwa katika karantini ya lazima nchini Kenya wamefanya mgomo na kutishia kutoroka katika kituo hicho katika mji mkuu wa Nairobi. Wanadai kwamba kusalia kwao katika vituo hivyo si haki kwa kuwa wamepimwa mara mbili na kukosekana kuwa na virusi hivyo.
Wiki iliopita, serikali ilitangaza kwamba muda wao wa kusalia karantini utaongezwa kutoka wiki mbili hadi mwezi mmoja baada ya kupatikana wakikaidi baadhi ya maagizo ya serikali kukabiliana na virusi vya corona.
Lakini kati ya wale walio katika karantini wanasema kwamba wanaugua shinikizo la kiakili. Kundi hilo la watu 21 ambalo limekuwa likiishi katika chuo kikuu cha Knyatta University liliagiza kusalia katika karantini baada ya vipimo vya hivi karibuni kuwapata wawili wao na virusi.
Hatua hiyo inajiri huku Kenya ikiripoti wagonjwa wengine tisa wa virusi vya corona na kufanya idadi ya wagonjwa waliopatikana na ugonjwa huo kufikia 225. Kulingana na waziri wa Afya, Mutahi Kagwe, maambukizi hayo mapya yaliripotiwa baada ya sampuli 803 kufanyiwa vipimo katika kipindi cha saa 24 zilizopita.
Wagonjwa wote ni Wakenya, hakuna aliye na historia ya kusafiri wala aliyetoka katika kituo cha karantini. Wagonjwa watano wanatoka Nairobi huku wanne wakitoka Mombasa.
Wana kati ya umri wa miaka tisa na 69. Hata hivyo, Kagwe amesema kwamba kuna habari njema baada ya wagonjwa 12 kupona na kuachiliwa kurudi nyumbani, hatua inayofanya idadi ya waliopona kwa jumla kufikia watu 53.
Mgonjwa mmoja ameripotiwa kufariki na kuongeza idadi ya waliofariki kutokana na virusi hivyo kufikia watu 10. Waziri huyo amesema kwamba takriban watu 2,336 waliokaribiana na wagonjwa hao wanachunguzwa huku 455 kati yao wakifuatiliwa.
