
UONGOZI wa Kampuni ya Global Publishers umetoa tuzo maalum kwa kundi la wanafunzi 30 kutoka katika Chuo Kikuu cha Tumaini na Chuo kikuu cha Dar es Salaam vitivo vya uandishi wa habari na mawasiliano ya umma waliokuwa wakifanya mafunzo kwa vitendo baada ya kumaliza mafunzo yao katika Kampuni hiyo.
Tuzo hiyo imetolewa leo Alhamisi na Mhariri Mtendaji wa Kampuni hiyo, Saleh Ally ‘Saleh Jembe’ kwa wanafunzi katika hafla fupi ya kuwaaga wanafunzi hao waliodumu kwenye mafunzo yao kwa vitendo kwa muda wa wiki nane.

Jembe ametumia nafasi hiyo ya kuwaaga kwa kuwashukuru na kuwapongeza kutokana na kuonyesha uwezo mkubwa katika mafunzo yao.
“Nitumie nafasi hii kuwapongeza wanafunzi wote wa ‘field’ waliopata nafasi ya kuja hapa Global kujifunza kiukweli mumenishangaza kwa utofauti mkubwa ambao mumeonyesha.
“Niwapongeze sana vijana wote, kiukweli mmefanya vizuri sana, uwezo wenu wa kubadilika kutokana na mazingira umekuwa wa hali ya juu sana.
“Nimepokea pongezi zenu juu ya namna ambavyo naweza kuwa rafiki na kiongozi kwa wakati mmoja, niseme hiyo ndiyo imekuwa tabia yangu na nitakufa nikiwa hivyo.

“Lakini niwapongeze wafanyakazi wote wa Global Publishers kwa kuweza kuishi vizuri na nyinyi na kuwapa ushirikiano mkubwa, hii ndiyo asili yetu na tutakuwa hivyo siku zote.

“Nimeandaa hii tuzo kwa wanafunzi wa vyuo vyote, lakini kwa kuwa wale wa Tumaini wapo wengi, watapata nafasi ya upendeleo na wataondoka nayo hii tuzo ili ikawe kumbukumbu bora katika maisha yao ya chuo, kuwa tuliwahi kufanya ‘field’ Global na tukapewa hii tuzo kama ishara ya utendaji kazi mzuri.

“Nimalize kwa kusema kuwa hapa ni nyumbani kwenu, mnakaribishwa wakati wowote mkihitaji kurudi. Ila ombi letu mkawe mabalozi wazuri huko muendako na kwa wale waliobahatika kupata nafasi ya kubaki, hakuna kulala ni mwendo wa kupiga kazi tu,” alisema Jembe.
Saleh Ally akiwakabidhi tuzo ya heshima wawakilishi wa wanafunzi wa Chuo cha Tumaini University Dar es Salaam College Turdaco, Wlifred John kushoto na Glory Olomi kulia.






