Msimamizi wa Uchaguzi jimbo la Moshi Mjini, amemtangaza Priscus Tarimo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa Mbunge wa Jimbo la Moshi Mjini baada ya kupata kura 31,169 akimshinda Raymond Mboya wa Chadema aliyepata kura 22,555.
Chama cha Mapinduzi kimefanikiwa kushinda nafasi ya ubunge katika Jimbo hilo kwa mara ya kwanza ndani ya miaka 25 ya chaguzi za mfumo wa vyama vingi Tanzania.
Katika uchaguzi wa mwaka 1995, upinzani ishinda majimbo sita kati ya majimbo tisa mkoani Kilimanjaro ambayo ni Hai, Siha, Moshi Mjini, Moshi Vijijini, Vunjo, na Rombo huku CCM ikishinda majimbo ya Mwanga, Same Mashariki na Same Magharibi.
Lakini katika chaguzi za mwaka 2000 na 2010, CCM ilifanikiwa kushinda katika majimbo ya Siha na Moshi Vijijini lakini mwaka 2015 majimbo hayo yalirudi mikononi mwa upinzani.
Katika uchaguzi wa mwaka 2020, matokeo ambayo tayari yameshatolewa na NEC yanaonesha kuwa CCM imefanikiwa kushinda katika majimbo ya Hai na Moshi Mjini, lakini bado matokeo katika majimbo mengine hayajatangazwa.
Katika hatua nyingine, CCM imefanikiwa kushinda ubunge katika Jimbo la Mbeya Mjini ambalo kwa miaka 10 limekuwa likishikiliwa na mbunge wa CHADEMA
