×

Mahakama Kuboresha Maslahi ya Watumishi

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akisalimiana na Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara na Mahakama ya wilaya ya Babati mara baada ya kuwasili mahakamani hapo.

Watumishi wote wa Mahakama nchini wenye nia ya kutaka kuhama na kwenda kwenye Taasisi nyingine za Serikali kwa lengo la kutafuta mazingira mazuri ya kufanyia kazi wameshauriwa kutokufanya hivyo kwa kuwa Mhimili huo umedhamiria na unaendelea kuboresha mazingira ya kazi pamoja na maslahi ya watumishi wake.

 

 

Baadhi ya Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara na Mahakama ya wilaya ya Babati wakimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel ameyasema hayo jana alipokuwa akizungumza na watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara pamoja na Mahakama ya wilaya ya Babati akiwa katika ziara yake ya kikazi yenye lengo la kujitambulisha kwa watumishi wa Mahakama na kutoa maelekezo ya utendaji kazi.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akifuatilia Taarifa ya Utendaji kazi ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara wakati ikiwasilishwa na Afisa Tawala Bw. Christopher Msagati (hayupo pichani).

“Tunaboresha mazingira, wenye nia ya kuhama waache hayo mawazo, tutengeneze nyumba yetu kwani hakuna mtu wa kututengenezea. Nashauri hama unapodhani kuna umuhimu wa kufanya hivyo, usihame kwa kufuata mkumbo”, alisema prof. Ole Gabriel.

 

Aidha, Mtendaji Mkuu wa Mahakama amewataka watumishi wote wa Mahakama nchini kukwepa mambo matano muhimu ambayo ni rushwa na uzembe kazini, ubadhirifu wa mali za Umma, lugha zisizo na staha hasa kwa wateja wanaofika mahakamani, kubaguana na kuchelewesha kumalizika kwa mashauri pasipokuwa na sababu za msingi.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara na Mahakama ya wilaya ya Babati.

Prof. Ole Gabriel amewashauri watumishi hao kujiendeleza kielimu ikiwezekana hata nje ya taaluma zao ili kuwaongezea ujuzi mbalimbali utakaowezesha kuboresha utendaji kazi wao na akawataka viongozi wa Mahakama kutowazuia watumishi wanaotaka kujiendeleza kielimu. “Wakubwa kuweni na kauli nzuri kwa watumishi walio chini yenu, muwajali na kuheshimiana”, alisisitiza.

 

 

Waheshimiwa Mahakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara na Mahakama ya wilaya ya Babati wakiwa katika picha ya pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel .

Awali akisoma taarifa ya utendaji kazi wa Mahakama hiyo kwa niaba ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara, Afisa Tawala wa Mahakama hiyo Bw. Christopher Msagati alisema ili kuendana na kasi ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), Mahakama ya Tanzania haina budi kuweka Maafisa Tehama katika ngazi za mikoa ili kurahisisha na kuboresha utendaji kazi. Hivi sasa kazi za Tehama hufanywa na Maafisa waliopo kwenye ngazi za kanda.

Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara na Mahakama ya wilaya ya Babati wakiwa katika picha ya pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel .

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania anaendelea na ziara ya kukagua miradi ya ujenzi wa majengo ya Mahakama na kuzungumza na watumishi wa Mahakama kwa lengo la kujitambulisha. Tayari amekagua ujenzi wa majengo mbalimbali ya Mahakama na kuzungumza na watumishi wa Kanda ya Dodoma na Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara.

 

Na Lydia Churi-Mahakama

Leave a Comment