
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa leo Oktoba 3, 2021 amezungumza na Mabalozi ambao wataiwakilisha Tanzania katika nchi mbalimbali, ofisini kwa Waziri Mkuu, Mlimwa jijini Dodoma.
Katika Mazungumzo hayo, Waziri Mkuu amewataka mabalozi hao kutanguliza maslahi ya Taifa katika utekelezaji wa majukumu yao.

Amesema kuwa mabalozi hao wanapaswa kutekeleza falsafa ya Mheshimiwa Rais Samia ya kuona kazi zilizoratibiwa zinaendelea kutekelezwa kwa uadilifu mkubwa na uaminifu ili ziweze kutoa matokeo chanya katika kila kazi zinazofanyika.
Mabalozi hao ni Grace Olotu anayekwenda Sweden, Anisa Mbega anayekwenda India, Luteni Jenerali Yacub Mohammed anayekwenda Uturuki, Meja Generali Richard Makanzo anayekwenda Rwanda, Innocent Shiyo anayekwenda Ethiopia, Hoyce Temu Naibu Balozi Geneva na Togolani Mavura anayekwenda Korea Kusini.