
BAADHI ya wazee wa kabila la Wachagga wamelaani kauli ya Mbunge wa jimbo la Vunjo Dkt Charles Kimei aliyoitoa hivi karibuni Bungeni ya kuwa Wachaga ni watu wanaopenda magendo huku wakimtaka kuomba radhi na kuifuta kwenye kumbukukumbu za Bunge.
Mbali na hatua hiyo Wazee hao wakiongozwa na Mwenyekiti wao Raymnd Mushi wamekiomba chama kilichompa dhamana ya kuogombea ubunge katika jimbo la Vunjo kumchukulia hatua za kinidhamu kwani aliyoyasema Bungeni si yale waliyomtuma.
Katika tamko lao Wazee hao wamesema kauli hizo zimewashtua na kwamba walijipa muda ili kuona kwamba endapo atatoka hadharani mapema kutengua kauli hizo lakini kwa ukimya uliopo ni kuwa alimaanisha kauli hizo.
Mwenyekiti huyo akatoa rai kwa chama kilichompa dhamana mbunge Dkt Kimei ya kuchukua hatua za kinidhamu kwa kauli yake hiyo.
Suala la matumzi ya dawa za kulevya ikiwemo Gongo bangi na Mirungi nalo likaonekana kuichafua jamii ya maeneo hayo na kwamba hali hiyo imetokana na tatizo la ajira jambo ambalo si tatizo kwa Vunjo pekee bali Tanzania kwa ujumla wake.
Katika kipindi cha maswali na majibu wakati wa kikao cha bunge Dkt Kimei amenukuliwa akisema jimbo la Vunjo ni miongoni mwa majimbo ya mpakani yakiwa na changamoto tofauti akitaja Magendo huku akisindikiza na kauli kuwa unajua wachaga wanavyopenda Magendo.