
OFISA Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) CPA Nicodemus Mkama, amezitaka kampuni za uwekezaji, zikiwemo benki za biashara, benki za wananchi, kampuni za bima na mashirika ya umma kutumia vyema fursa za kujiongezea kipato.
Amezitaka kutumia fursa zilizopo katika sekta ya masoko ya mitaji, ikiwemo kuuza hisa na hatifungani kwa umma na hatimaye kuorodheshwa katika soko la hisa kwa lengo la kuongeza uwezo wa rasilimali fedha.

Mkama ameyasema hayo Desemba 14, 2023 jijini Dar es Salaam katika hafla ya kuorodheshwa kwa Hisa za upendeleo millioni 72 za Kampuni ya Uwekezaji ya TCCIA Investment Plc kwenye Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE).
“Ndugu wageni waalikwa, natoa wito kwa kampuni za uwekezaji, benki za biashara, benki za wananchi, kampuni za bima na mashirika ya umma kutumia fursa zilizopo katika sekta ya masoko ya mitaji, ikiwa ni pamoja na kuuza hisa na hatifungani kwa umma na hatimaye kuorodheshwa katika soko la hisa ili kuongeza uwezo wa rasilimali fedha,” amesema.
Ametoa rai kwa wadau wa masoko ya mitaji kuendelea kushirikiana na Serikali kupitia CMSA katika kutekeleza mikakati ya kuendeleza masoko ya mitaji nchini ikiwemo kuleta bidhaa mpya katika masoko ambazo zitaorodheshwa katika Soko la Hisa.

Ameongeza hiyo tawezekana ikiwa TCCIA pamoja na mambo mengine itahakikisha kuwa inatekeleza maelekezo ya Serikali kupitia Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) kwamba kiasi kilicho patikana kutokana na mauzo ya hisa kinatumika kuwekezwa kwa mujibu wa sera za uwekezaji zilizopitishwa na Bodi na kuidhinishwa na Mamlaka.
Pia uwekezaji sahihi utaiwezesha TCCIA kuongeza ufanisi wa kampuni na kupata faida na hivyo kuongeza thamani ya uwekezaji kwa wanahisa huku akisisitiza Mamlaka hiyo itaendelea kujenga mazingira wezeshi na shirikishi ili kuwezesha taasisi katika sekta ya umma na binafsi kutumia masoko ya mitaji kupata fedha za kutekeleza miradi na shughuli za maendeleo.
Ameongeza ambapo ni pamoja na kuuza hisa kwa umma, hatifungani za miundombinu (infrastructure bonds), hatifungani Rafiki wa mazingira (green bonds), hatifungani za bluu (blue bonds), na hatifungani za taasisi za Serikali (subnational bonds).
Pamoja na hayo amesema utoaji wa hisa za upendeleo unatoa fursa kwa wanahisa kuongeza uwekezaji wao kwa bei nafuu na hivyo kufaidika na punguzo la bei; na ni miongoni mwa njia zinazotumiwa na kampuni kuongeza mtaji.
Aidha, uorodheshwaji wa hisa za upendeleo za TCCIA Investment Plc katika soko la hisa unawapatia fursa wawekezaji kuuza hisa zao pale wanapohitaji fedha kwa ajili ya matumizi mengine; kujua thamani halisi ya hisa zao; na kuwapatia fursa wawekezaji wapya kununua hisa hizo.
“Nimefurahi kuona mikakati madhubuti iliyowekwa na Bodi na Uongozi wa TCCIA Investment Plc juu ya matumizi sahihi ya fedha zilizopatikana kupitia mauzo ya hisa, ambapo, fedha hizo zitatumika kukuza uwekezaji wa kampuni hii katika dhamana mbalimbali za masoko ya mitaji, ikiwa ni pamoja na kuwekeza katika hisa za kampuni, hatifungani na vipande katika mifuko ya uwekezaji wa pamoja. Alisema CPA, Mkama.