×

Wanachadema Walioshitakiwa Kwa Mauaji Waachiwa Huru

Mahakama Kuu Kanda ya Iringa imewaachia huru wanachama watatu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo  akiwemo aliyekuwa Katibu wa Jimbo George Sanga na wenzake Gudluck Mfuse na Octatus Mkwela kutokana na kutokutwa na hatia ya kuhusika na mauaji ya kada wa Chama cha Mapinduzi Emmanuel Mlelewa.

Akisoma hukumu hiyo kwa njia ya mtandao mkoani Njombe Jaji Mfawidhi Kanda ya Iringa Danstan Ndunguru amesema washtakiwa hao wameachiwa huru kutokana na upande wa jamhuri kushindwa kuthibitisha mashtaka yao.

Jaji Ndunguru amesema ushahidi pekee uliotolewa na mashahidi hao ni wa kimazingira kwani hakuna ambaye ameona washtakiwa hao wakifanya kosa hilo na mahakama kushindwa kujiridhisha kuwa washtakiwa hao wamefanya kosa.

“Ili uweze kuthibitisha ushahidi wa kimazingira lazima ujitosheleze lakini jamhuri imeshindwa kuthibitisha” amesema Jaji Ndunguru.

Amesema sababu nyingine iliyofanya washtakiwa hao kutokuwa na hatia ni baadhi ya mashahidi muhimu akiwemo mkuu wa upelelezi mkoa kushindwa kufika mahakamani.

Kwa upande wa mawakilii upande wa utetezi ukiongozwa na Dickson Matata na wenzake alisema kesi hiyo ilikuwa na mashahidi 14 upande wa jamhuri na 5 upande wa utetezi.

Amesema katika kesi hiyo namba 5236 ya mwaka 2024 kati ya mashahidi hao 14 hakuna hata mmoja aliyesema mahakamani kuwa amemuona mmoja kati ya washtakiwa hao akimuua Emmanuel Melwa.

“Kwenye kesi yetu hakuna mshtakiwa hapa aliyekiri… kwa kufuata utaratibu kukiri kuliozungumziwa mahakamani ni kwa shahidi polisi akiwa kwa RCO alimsikia George Sanga akikiri na kuwataja wenzake” amesema Matata.

Ikumbukwe Emmanuel Mlelwa alikuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi UVCCM kwa Mkoa wa Iringa aliuawa tarehe 21, Septemba 2020 mkoani Njombe.

Leave a Comment