Al Ahly Wamchapa Ashour Faini Kubwa, Agoma kwenda Zanzibar

Klabu ya Al Ahly ya Misri imemtoza kiungo wao nyota, Emam Ashour, faini kubwa zaidi kuwahi kutolewa katika historia ya klabu hiyo, kufuatia kushindwa kwake kusafiri na kikosi kwenda Zanzibar kwa ajili ya mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Yanga.
Kupitia taarifa rasmi, Al Ahly imethibitisha kuwa Ashour amepigwa faini ya pauni milioni 1.5 za Misri (EGP 1.5m), kiasi kinachovunja rekodi ya awali ya faini ya EGP milioni 1, ambayo pia iliwahi kutolewa kwa mchezaji huyo pamoja na Mahmoud Kahraba katika matukio ya nyuma.
Mbali na faini hiyo, Mkurugenzi wa Soka wa Al Ahly, Walid Salah El-Din, ameagiza Ashour kusimamishwa kwa wiki mbili kwa kosa la kushindwa kuambatana na timu wakati wa safari ya Alhamisi asubuhi kuelekea Zanzibar kwa ajili ya mchezo huo wa CAF Champions League.
Klabu imesema Emam Ashour atafanya mazoezi binafsi kwa kipindi chote cha kusimamishwa, na hataruhusiwa kushiriki mazoezi ya pamoja ya kikosi hadi Februari 12.
Al Ahly wanatarajiwa kuikabili Yanga siku ya kesho Jumamosi saa 10:00 jioni, katika Uwanja wa Amaan Stadium, Zanzibar, ikiwa ni mchezo wa raundi ya nne ya hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Katika mchezo wa awali (raundi ya tatu), Al Ahly waliibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Yanga katika Uwanja wa Borg El Arab, mjini Alexandria.
Kwa sasa, Al Ahly wanaongoza Kundi B wakiwa na pointi 7, huku Young Africans wakiwa nafasi ya pili na pointi 4, hali inayoufanya mchezo wa Zanzibar kuwa muhimu katika mbio za kuwania kufuzu hatua inayofuata.

