
Rais wa Marekani Donald Trump na Rais wa China Xi Jinping wamekubaliana kwamba njia muhimu ya mafuta duniani ya Strait of Hormuz lazima ibaki wazi huku mvutano wa kijeshi unaohusisha Iran ukiendelea kuibua hofu duniani.
Kwa mujibu wa taarifa ya Ikulu ya Marekani (White House) baada ya mkutano wa viongozi hao mjini Beijing, pande zote mbili zimesisitiza umuhimu wa kulinda mtiririko wa nishati duniani kupitia njia hiyo muhimu ya baharini. Viongozi hao pia walikubaliana kuwa Iran haipaswi kamwe kumiliki silaha za nyuklia.

Kauli hiyo imekuja wakati hali ya usalama katika Ghuba ya Uajemi ikiendelea kuzorota, huku taarifa zikieleza kuwa meli kadhaa zimevamiwa au kushambuliwa karibu na eneo la Strait of Hormuz. Shirika la usalama wa baharini la Uingereza lilisema meli moja ilichukuliwa na watu wasiojulikana karibu na pwani ya UAE na kuelekezwa kwenye maji ya Iran.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Abbas Araghchi, alisema njia hiyo bado iko wazi kwa meli za kibiashara lakini akasisitiza kuwa meli hizo zinapaswa kushirikiana na vikosi vya majini vya Iran.
Wakati huo huo, China imeripotiwa kufanya mazungumzo na Tehran ili kuhakikisha baadhi ya meli zake zinaendelea kupita katika njia hiyo muhimu ya biashara ya mafuta duniani.

Katika upande mwingine wa mgogoro huo, jeshi la Israel limesema raia kadhaa wamejeruhiwa baada ya shambulio la ndege isiyo na rubani lililorushwa na Hezbollah karibu na mpaka wa Lebanon. Israel nayo imejibu kwa kufanya mashambulizi katika maeneo ya kusini mwa Lebanon.
Mvutano huo umeanza pia kuathiri uchumi wa dunia, huku bei za mafuta zikiongezeka na kuathiri matumizi ya watumiaji katika baadhi ya nchi, ikiwemo Marekani.
Strait of Hormuz ni moja ya njia muhimu zaidi duniani kwa usafirishaji wa mafuta, ambapo takribani asilimia 20 ya mafuta yanayosafirishwa duniani hupitia eneo hilo. Hofu ya kuzuiwa kwa njia hiyo imeendelea kuzua wasiwasi mkubwa katika masoko ya kimataifa.