
Rais wa Colombia anayemaliza muda wake, Gustavo Petro, ameibua mashaka kuhusu mchakato wa uchaguzi nchini humo baada ya matokeo ya awali kumuweka mgombea wake kipenzi, Iván Cepeda, akielekea duru ya pili ya uchaguzi dhidi ya mpinzani wake wa mrengo wa kulia, Abelardo de la Espriella.
Kwa mujibu wa matokeo ya awali yaliyohesabiwa kwa asilimia 100 ya kura, De la Espriella ameongoza kwa zaidi ya asilimia 43, huku Cepeda akiwa nyuma kwa takriban asilimia 40. Hakuna mgombea aliyefikisha asilimia 50 inayohitajika kushinda moja kwa moja, hivyo duru ya pili itafanyika Juni 21.
Petro, ambaye ameunga mkono wazi Cepeda, amesema hawezi kukubali matokeo ya awali akidai kuwa mfumo wa kidijitali wa kuhesabu kura unaotumiwa na makampuni binafsi una dosari. Pia alidai kuwa kuna namba za kitambulisho zaidi ya 800,000 zilizoingizwa kwenye mfumo bila uwepo katika orodha rasmi ya wapiga kura, ingawa hakutoa ushahidi wa madai hayo.

Cepeda naye alionyesha mashaka, akisema kulikuwa na makosa katika uhesabuji wa kura na tofauti katika takwimu zilizotolewa. Alisisitiza haja ya uhakiki wa kina wa matokeo.
Hata hivyo, mamlaka ya uchaguzi nchini Colombia imeeleza kuwa mfumo wa uchaguzi ni huru na wa kuaminika, huku wachunguzi wa haki za binadamu wakikosoa kauli za rais wakisema zinahatarisha imani ya umma katika mchakato wa kidemokrasia.
Uchaguzi huu umegeuka kuwa ushindani mkali kati ya mirengo miwili tofauti ya kisiasa. De la Espriella, ambaye amejijengea sifa kama mwanasiasa wa nje ya mfumo na muungaji mkono wa sera kali za kupambana na uhalifu, amejipambanua kama mshirika wa siasa za Donald Trump na ameahidi hatua kali dhidi ya makundi ya kihalifu.

Kwa upande mwingine, Cepeda, seneta wa mrengo wa kushoto na mshirika wa Petro, amejikita katika sera za mazungumzo na makundi yenye silaha pamoja na mageuzi ya kijamii na kiuchumi.
Duru ya pili ya uchaguzi inatarajiwa kuwa na athari kubwa kwa mustakabali wa Colombia, hasa katika sera za usalama, mapambano dhidi ya dawa za kulevya, na uhusiano wa nchi hiyo na Marekani na majirani zake wa Amerika Kusini.
