
Kampuni ya mawasiliano ya Airtel Tanzania imeendelea kuonesha dhamira yake ya kuchangia maendeleo ya jamii kwa kuunganisha ajenda za afya, ustawi wa wafanyakazi na uhifadhi wa mazingira kupitia udhamini wake wa mbio za Great Ruaha Marathon 2026, zilizofanyika ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Ruaha, mkoani Iringa.
Ikiwa mdhamini rasmi kutoka sekta ya mawasiliano, Airtel ilishiriki pamoja na mamia ya wakimbiaji katika tukio hilo ambalo limeendelea kujijengea sifa kama moja ya mbio za kipekee nchini zinazochanganya michezo, utalii na juhudi za kuhifadhi mfumo wa ikolojia wa Mto Mkuu wa Ruaha.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkurugenzi wa Rasilimali Watu wa Airtel Tanzania, Stellah Kibaja, alisema ushiriki wa kampuni hiyo unaakisi dhamira ya kuleta mchango chanya kwa jamii sambamba na shughuli zake za kibiashara.
“Airtel tunaamini mahusiano imara hayajengwi kupitia mtandao wetu pekee, bali kupitia watu, uzoefu wa pamoja na jamii zinazounganishwa na lengo moja.
Ndiyo maana tunajivunia kuwa sehemu ya Great Ruaha Marathon, tukio linaloendana na maadili yetu ya kuhamasisha afya bora, kuunga mkono jamii na kushiriki katika mipango yenye manufaa ya kudumu,” alisema Kibaja.
Katika kuonesha mfano wa uongozi unaoshiriki kwa vitendo, Airtel iliwashirikisha wafanyakazi 20 katika mbio hizo, wakiwemo wajumbe watatu wa Kamati ya Utendaji ya kampuni hiyo.
Kibaja alisema afya ya wafanyakazi ni msingi muhimu wa mafanikio ya taasisi yoyote, akisisitiza kuwa watu wenye afya hujenga timu imara, ambazo huleta mafanikio ya biashara na kuchangia maendeleo ya jamii.
Aliongeza kuwa Airtel imeendelea kuwekeza katika programu mbalimbali za ustawi wa wafanyakazi zinazolenga kuimarisha afya ya mwili na akili pamoja na kuweka uwiano mzuri kati ya kazi na maisha binafsi, hatua inayoongeza tija kazini na kuboresha huduma kwa wateja.
Mbali na kuhamasisha afya kupitia michezo, Airtel imeendelea kuunganisha mamilioni ya Watanzania kupitia huduma za sauti, intaneti, Airtel Smart Box na Airtel Money, huku ikiendelea kupanua mtandao wake hadi maeneo ya vijijini ili kuongeza upatikanaji wa huduma za kidijitali.
Akihitimisha, Kibaja aliwahimiza washiriki wa mbio hizo kuona tukio hilo kama jukwaa la kuleta mabadiliko chanya kwa kuwekeza katika afya zao, kuunga mkono uhifadhi wa mazingira na kushiriki katika juhudi za maendeleo ya jamii.
Great Ruaha Marathon imeendelea kukua na kuwa jukwaa muhimu linalovutia ushiriki wa sekta binafsi katika kuhamasisha afya, kukuza utalii endelevu na kuimarisha uhifadhi wa ikolojia ya Mto Mkuu wa Ruaha, ambao una mchango mkubwa katika uhifadhi wa mazingira na uzalishaji wa nishati nchini.