
Kylian Mbappé amemkosoa vikali seneta wa Paraguay, Celeste Amarilla, kufuatia kauli alizozieleza mitandaoni ambazo zimeelezwa kuwa za kibaguzi baada ya Paraguay kuondolewa na Ufaransa katika hatua ya 16 bora ya Kombe la Dunia.
Mbappé, kupitia akaunti yake ya X siku ya Jumatatu, alimuita Amarilla “mwanamke wa kudharaulika” na kusema hastahili kuwa mjumbe wa Bunge la Paraguay.
“Kutokana na uzembe wako na ubaguzi wako wa wazi, dunia yote tayari imesahau safari na juhudi za kihistoria zilizofanywa na wachezaji wa Paraguay katika Kombe hili la Dunia,” aliandika nahodha huyo wa Ufaransa.
Mzozo huo ulianza baada ya Amarilla kuchapisha ujumbe kadhaa wa kibaguzi akimshambulia Mbappé kufuatia kufunga penalti ya ushindi iliyoivusha Ufaransa kwenda robo fainali. Katika machapisho hayo, alimkejeli nyota huyo kwa asili yake, malezi, elimu na hata muonekano wake.
Baadaye Jumatatu, Amarilla alitoa barua ya wazi kwa lugha za Kifaransa na Kihispania akisema tatizo lake lilikuwa na Mbappé binafsi, si taifa la Ufaransa. Alikiri kujutia kutumia matusi aliyodai yeye mwenyewe amewahi kuyapokea kama mtu mwenye asili ya mchanganyiko wa rangi, na kuthibitisha kuwa amefuta chapisho lake.

Hata hivyo, seneta huyo pia alimtaka Mbappé amuombe radhi, akidai kauli zake zilikuwa na dhuluma dhidi ya wanawake, na kutishia kuchukua hatua za kisheria iwapo hatarudisha kauli hizo.
Serikali ya Paraguay ilitoa tamko ikilaani matamshi ya Amarilla, ikisema yanapingana na misingi ya heshima kwa utu wa binadamu na hayawakilishi serikali wala wananchi wa Paraguay.
Kwa upande wake, French Football Federation ilielezea kauli hizo kuwa “za kuchukiza kabisa” na “zisizokubalika,” huku ikitangaza kuwa suala hilo litapelekwa kwa waendesha mashtaka.
Rais wa France, Emmanuel Macron, pamoja na Waziri wa Michezo, Marina Ferrari, walionesha kumuunga mkono Mbappé.
Macron aliandika kwenye X: “Bao lingine kwa Kylian Mbappé. Safari hii dhidi ya ubaguzi wa rangi,” akisisitiza kuwa nahodha huyo anaungwa mkono kikamilifu na serikali ya Ufaransa.
Naye kocha msaidizi wa Ufaransa, Guy Stephan, alizitaja kauli hizo kuwa “za kusikitisha, za aibu na za fedheha.”
Kabla ya mchezo huo, kipa wa zamani wa Paraguay, José Luis Chilavert, pia aliibua mjadala baada ya kudai kuwa timu ya Ufaransa ni “kikosi kutoka Afrika,” kauli iliyolaaniwa na rais wa Shirikisho la Soka la Ufaransa, Philippe Diallo.