×

Infantino: Kombe la Dunia 2026 Limefanikiwa Kuunganisha Dunia

Rais wa Shirikisho la Soka Duniani (FIFA), Gianni Infantino, amesema Kombe la Dunia la FIFA 2026 limekuwa mafanikio makubwa kwa kutimiza lengo lake la kuwaleta pamoja watu kutoka mataifa mbalimbali duniani.

Akizungumza katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa (UN) jijini New York wakati wa kikao kilichojadili mchango wa soka katika afya ya akili ya vijana, Infantino alisema mpira wa miguu ni lugha ya kimataifa inayounganisha watu licha ya tofauti zao.

Akiwa ameshika moja ya mipira rasmi itakayotumika kwenye fainali ya Kombe la Dunia kati ya Argentina na Hispania Jumapili, alisema mpira huo ni “kitu cha kipekee chenye uwezo wa kuiunganisha dunia.”

“Tunaambiwa mara nyingi kuwa dunia imegawanyika na imejaa migogoro, lakini Kombe hili la Dunia limetuonyesha kuwa mambo yanayotuunganisha ni mengi zaidi kuliko yanayotugawa,” alisema Infantino.

Kombe la Dunia la 2026 limeandika historia kwa kushirikisha timu 48 kwa mara ya kwanza, huku mechi zikichezwa nchini Marekani, Canada na Mexico. FIFA imesema viwanja karibu vyote vimejaa mashabiki katika mechi 102 zilizochezwa hadi sasa, huku jumla ya watazamaji ikitarajiwa kufikia takribani milioni 6.7, rekodi mpya katika historia ya mashindano hayo.

Infantino alisema mamilioni ya mashabiki kutoka duniani kote wamekusanyika kwa amani na furaha kusherehekea mchezo huo, jambo alilosema linapaswa kuwa msingi wa kujenga dunia yenye umoja na mshikamano.

Licha ya mafanikio hayo, mashindano hayo yamekumbwa na mijadala mbalimbali ikiwemo changamoto za kisiasa. Timu ya Iran ilikabiliwa na vikwazo vya usafiri kutokana na vita vinavyoendelea kati ya Iran na Marekani, huku FIFA pia ikikosolewa baada ya kuondoa adhabu ya kadi nyekundu kwa mshambuliaji wa Marekani Folarin Balogun. Aidha, Serikali ya Uingereza imeitaka FIFA kuchunguza timu ya Argentina baada ya wachezaji wake kuonyesha bendera iliyodai umiliki wa Visiwa vya Falkland kufuatia ushindi wao dhidi ya England.

Infantino aliahidi kuwa FIFA itaendelea kushirikiana na Umoja wa Mataifa kuunga mkono juhudi za kuboresha afya ya akili kwa vijana, akisisitiza kuwa soka lina uwezo mkubwa wa kuvuka mipaka ya lugha, tamaduni na siasa.

“Baada ya siku mbili tutajua kama Argentina au Hispania watakuwa mabingwa wa dunia, lakini jambo tunalolijua tayari ni kwamba soka si mchezo maarufu pekee duniani, bali limekuwa lugha ya pamoja inayowaunganisha watu wote,” alisema.

Leave a Comment