
Marekani imefanya mashambulizi mapya ya anga dhidi ya Iran baada ya shambulio lililolenga kambi ya kijeshi ya Marekani nchini Jordan kuwaua wanajeshi wawili wa Marekani, mmoja kutoweka na wengine wanne kujeruhiwa.
Kwa mujibu wa Kamandi Kuu ya Jeshi la Marekani (CENTCOM), mashambulizi hayo yalifanyika Jumapili jioni kwa amri ya Rais Donald Trump, yakilenga “kuadhibu haraka” vikosi vya Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) vinavyodaiwa kuhusika na shambulio hilo.
Jeshi la Marekani limesema mashambulizi hayo pia yanalenga kudhoofisha uwezo wa Iran wa kutishia usafirishaji wa meli katika Mlango wa Hormuz, njia muhimu inayobeba sehemu kubwa ya mafuta ya dunia.
Wakati huo huo, vyombo vya habari vya Iran vilidai kuwa vikosi vya nchi hiyo vilifanya mashambulizi ya ndege zisizo na rubani dhidi ya kambi za Marekani nchini Kuwait, zikilenga ghala la silaha katika Camp Udairi pamoja na mifumo ya rada katika Kambi ya Ali Al Salem. Iran pia ilidai kushambulia kambi ya Chama cha Kurdistan Freedom Party karibu na mji wa Irbil nchini Iraq.
Tangu kuanza kwa vita hivyo, Marekani imesema wanajeshi wake 16 wameuawa huku zaidi ya 430 wakijeruhiwa. Waziri wa Ulinzi wa Marekani Pete Hegseth aliwapa heshima wanajeshi waliopoteza maisha akisema, “Dhabihu yao inaimarisha azma yetu.”
Katika upande mwingine, vyombo vya habari vya Iran viliripoti kuwa mashambulizi ya Marekani yalilenga maeneo ya Sirik, Hajjiabad, Bandar Abbas na karibu na Kisiwa cha Qeshm kusini mwa Iran. Serikali ya Iran ilisema hakuna uharibifu mkubwa ulioripotiwa katika baadhi ya maeneo hayo, ingawa mashambulizi ya siku za nyuma yameharibu madaraja, njia za usafiri na miundombinu ya umeme.
Iran pia imesema watu wasiopungua 50 wameuawa na zaidi ya 500 kujeruhiwa kutokana na mashambulizi ya Marekani ndani ya kipindi cha wiki tatu zilizopita.
Wakati mvutano huo ukiendelea kuongezeka, kiongozi mkuu wa Iran, Mojtaba Khamenei, alionya kuwa Marekani itapata “funzo lisilosahaulika” ikiwa itaendelea na mashambulizi dhidi ya Iran. Aidha, Tehran imetangaza kusitisha utekelezaji wa makubaliano ya muda ya kusitisha mapigano yaliyokuwa yamefikiwa mwezi mmoja uliopita.
Kuongezeka kwa mapigano hayo kunaendelea kuzua hofu ya kurejea kwa vita kamili kati ya Marekani na Iran, huku usalama wa usafirishaji wa mafuta kupitia Mlango wa Hormuz na uthabiti wa uchumi wa dunia ukiendelea kuwa mashakani.