×

Messi Avunja Ukimya Baada ya Kupoteza Fainali ya Kombe la Dunia

Lionel Messi amefunguka kuhusu maumivu aliyopata baada ya Argentina kupoteza fainali ya Kombe la Dunia 2026 dhidi ya Hispania, huku kukiwa na uwezekano kuwa ilikuwa mechi yake ya mwisho kwenye michuano hiyo mikubwa duniani.

Messi alionekana akiwa na machozi uwanjani baada ya Argentina kushindwa kutwaa ubingwa wa pili mfululizo, na baadaye aliandika ujumbe kupitia ukurasa wake wa Instagram akisema maumivu ya kupoteza fainali ni makubwa na yatachukua muda kupona.

“Maumivu ni makubwa sana, na jeraha hili litachukua muda kupona. Lakini pia nitaendelea kushikilia kumbukumbu zote nzuri,” aliandika Messi.

Nyota huyo wa Argentina alisisitiza kuwa licha ya kushindwa kutetea ubingwa walioutwaa mwaka 2022 nchini Qatar, timu yao imefanya jambo kubwa kwa kufika fainali mbili za Kombe la Dunia mfululizo.

“Ni vigumu kuthamini kikamilifu mafanikio yetu kwa sasa, lakini kikosi hiki kimefika fainali mbili mfululizo za Kombe la Dunia,” alisema.

Argentina ilipoteza fainali ya 2026 kwa Hispania baada ya kushindwa kupata bao katika mchezo ambao ulinzi wa Hispania uliwazuia kabisa washambuliaji wa Argentina. Awali, Argentina ilikuwa imetwaa Kombe la Dunia 2022 baada ya kuifunga Ufaransa kwa mikwaju ya penalti kufuatia sare ya 3-3.

Messi, ambaye alitimiza miaka 39 wakati wa michuano hiyo, hakutoa kauli rasmi kuhusu kama ataendelea kucheza Kombe la Dunia au la. Hata hivyo, Kombe la Dunia la 2030 litakapofanyika Hispania, Ureno na Morocco atakuwa na umri wa miaka 43.

Mbali na kuishukuru Argentina kwa kumuunga mkono, Messi pia aliipongeza Hispania kwa kutwaa ubingwa.

Katika Kombe la Dunia 2026, Messi alivunja rekodi ya Miroslav Klose ya mabao mengi ya muda wote katika Kombe la Dunia, akifikisha mabao 21, ingawa baadaye alizidiwa na Kylian Mbappé aliyefikisha mabao 22.

Kwa sasa, Messi na mwenzake wa timu ya taifa na klabu ya Inter Miami, Rodrigo De Paul, wanatarajiwa kupumzishwa katika mechi mbili zijazo za ligi ya Marekani (MLS) pamoja na mchezo wa MLS All-Star ili kupata muda wa kupona baada ya mashindano hayo.

Leave a Comment