×

Trump Ataka Saudi Arabia Kuingia Kwenye Mkataba wa Amani Kabla ya Nyuklia

Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema uidhinishwaji wa mkataba unaopendekezwa wa ushirikiano wa nyuklia kwa matumizi ya kiraia kati ya Marekani na Saudi Arabia utategemea iwapo Riyadh itaamua kujiunga na Makubaliano ya Abraham (Abraham Accords).

Katika ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wake wa Truth Social, Trump amesema makubaliano hayo yanahusu ushirikiano wa nyuklia kupitia Wizara ya Nishati ya Marekani na Saudi Arabia kwa matumizi ya kiraia pekee.

Amesisitiza kuwa mkataba huo hautaruhusu urutubishaji wa nyenzo za nyuklia kwa madhumuni ya kijeshi, bali utalenga matumizi ya amani kama uzalishaji wa nishati.

Trump amesema makubaliano hayo yanafanana na mikataba ambayo Marekani tayari imeingia na mataifa mengine, ikiwemo Iran na Falme za Kiarabu (UAE), akieleza kuwa Marekani inaunga mkono matumizi ya teknolojia ya nyuklia kwa maendeleo ya kiraia.

Hata hivyo, rais huyo amesema mkataba huo utaidhinishwa kwa sharti Saudi Arabia ijiunge na Makubaliano ya Abraham, ambayo ameyataja kuwa ni makubaliano yenye “heshima kubwa na mafanikio.”

Trump pia amesisitiza kuwa Marekani haina pingamizi dhidi ya programu za nyuklia za kiraia, mradi tu zisihusishe urutubishaji wa nyenzo za nyuklia kwa ajili ya silaha.

Leave a Comment