×

Trump Akanusha Marekani Kuishiwa Silaha, Aonya Watu Wanaovuja Siri za Serikali

Rais wa Marekani, Donald Trump, amekanusha taarifa zinazodai kuwa Marekani inakabiliwa na upungufu wa silaha na risasi za kijeshi, akisema nchi hiyo bado ina akiba kubwa ya zana za kivita.

Trump alisema kupitia mitandao ya kijamii kuwa Marekani inaendelea kuzalisha silaha na pia kuagiza nyingine kulingana na mahitaji yake.

“Marekani ina akiba kubwa ya silaha na risasi. Zaidi ya hayo, tunaendelea kutengeneza huku zingine zikiletwa nchini kulingana na mahitaji yetu,” aliandika Trump.

Kauli hiyo imekuja wakati vita kati ya Marekani na Iran vikiingia mwezi wa sita, huku kukiwa na mjadala kuhusu uwezo wa Marekani kuendelea na operesheni za kijeshi kwa muda mrefu bila kuathiri akiba yake ya silaha.

Ripoti za vyombo vya habari vya Marekani zimeeleza kuwa Washington imetumia kiasi kikubwa cha baadhi ya makombora yake ya masafa marefu katika mzozo huo, hali iliyozua maswali kuhusu viwango vya akiba ya silaha za jeshi la Marekani.

Trump pia ameonya kuwa watu watakaobainika kuvujisha taarifa za siri za serikali watakabiliwa na hatua kali za kisheria, akisema utawala wake utatafuta “hukumu za muda mrefu gerezani” kwa wahusika.

Wakati huo huo, licha ya kuwepo kwa majaribio kadhaa ya kusitisha mapigano kati ya Marekani na Iran, mashambuliano yameendelea huku juhudi za kufikia makubaliano ya kudumu zikiwa bado hazijafanikiwa.

Leave a Comment