
AZAM FC imepanga kucheza mchezo mmoja wa kirafiki katika kujiandaa na mchezo wa Robo Fainali ya Kombe la FA dhidi ya Mtibwa Sugar.
Mchezo huo unatarajiwa kuchezwa Jumamosi hii kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.
Azam iliingia kambini wiki iliyopita kujiandaa na mchezo huo na Mtibwa ambao utachezwa Machi 31, mwaka huko Azam Complex.
Akizungumza na Championi Jumatano, Ofisa Habari wa Azam, Jaffar Idd alisema kuwa timu hiyo inaendelea kujifua kujiwinda na mchezo huo unaotarajiwa kuwa mgumu na upinzani kutokana na ubora waliokuwa nao Mtibwa.
Jaffar alisema, timu hiyo watakayocheza nayo mchezo wa kirafiki wataitangaza hivi karibuni baada ya kufikia makubaliano mazuri.
“Tunatarajia kucheza mchezo mmoja wa kirafiki siku ya Jumamosi ni maalum kwa ajili ya kocha kuwaangalia wachezaji wake kama wameshika mafunzo na maelekezo ambayo amekuwa akiwapatia.
“Mazoezi pekee hayatoshi kwa wachezaji, hivyo ni lazima tucheze mechi kwa ajili ya kuwapima nguvu, kwani hivi sasa nguvu zetu zote tumezielekeza huko kwenye FA, licha ya kuwa na nafasi ya ubingwa wa ligi,” alisema Jaffer.