RAIS John Magufuli amesema alimuagiza Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Albert Chalamila kuwafukuza shule wanafunzi wote wa kidato cha tano na sita wa Shule ya Sekondari Kiwanja iliyopo Chunya na kuivunja bodi ya shule hiyo baada ya wanafunzi hao kukamatwa na simu za mkononi na kuchoma moto mabweni Oktoba 1, 2019.
Magufuli amesema hayo leo Ijumaa, Oktoba 4, 2019, wakati akizungumza na wananchi wa Songwe katika ziara yake ya siku nne, mkoani humo ambayo ameianza leo.

“Nampongeza RC wa Mbeya (Chalamila), kwa wale watoto waliotimuliwa shuleni lazima wazazi wao walipe. Nasema haya si kwamba sina huruma, nimeshawahi kuwa mwalimu, nafikiri kuna mahali tumekosea hii sheria kuhusu viboko.
“Baba wa Taifa aliwazungumzia maadui watatu ambao ni ujinga, maradhi na umaskini na bado hawajabadilika, hawa ni maadui wakubwa katika maendeleo yetu. Kila awamu ilijaribu, na awamu hii pia bado inajitahidi kukabiliana na hao maadui.
“Naagiza uongozi wa Jimbo la Mbozi, kuacha mara moja kuchangisha wananchi michango ya shule ya msingi Mahanje, Sh 25,000 badala yake ibaki Sh 3,000 ya awali. Nakabidhi shilingi milioni tano kwa ajili ya mchango was shule hiyo, hivyo msiwasumbue wananchi tena.
“Miradi niliyozindua leo imenifurahisha, nimeshawishika baada ya kupata maelezo mazuri ya watendaji hivyo nimeagiza wanunue mashine nyingine ili kuwe na uzalishaji mkubwa wa maji hapa.
“Naomba zitengwe ekari 50 kwa ajili ya kujenga stendi ya mkoa na soko la mazao. Ikiwezekana kuanzia wiki ijayo muwe mmeshakata hilo eneo na muweke alama stendi iliyopo, kwani sasa ni ndogo sana, hata magari hayawezi kutoka Zambia yakaja kupaki kwenye hako ka-stendi.
“Kiwanda hiki kimetengenezwa na kijana mdogo sana, hii ndio maana halisi ya Tanzania ya viwanda, nampongeza sana kijana huyu na tunahitaji vijana kama huyu na ningekuwa na binti ningemuozesha,” amesema Magufuli.