Ghorofa Laporomoka Goba, Wanne Wafariki – Video
WATU wanne wamefariki dunia na wengine 17 kujeruhiwa baada ya jengo la ghorofa kuporomoka katika Kata ya Goba Manispaa ya Ubungo jijini Dar es Salaam.
Mkuu wa Wilaya ya Ubungo (DC), Kheri James leo Jumatatu Desemba 6, 2021 amethibitishha kutokea kwa ajali hiyo, akisema baada ya jengo hilo lililokuwa linajengwa kuanguka limesababisha maafa kwenye nyumba zilizopo jirani.
“Katika ajali hii tunazo maiti nne, wanawake wawili na wanaume wawili na majeruhi wapo 17 waliopata majanga kutokana na jengo hili kuanguka” amesema DC James akiwa kwenye eneo la tukio.
Amesema kuwa vyombo vya ulinzi na usalama vipo katika eneo la tukio vikichukua hatua kuhakikisha kama kuna maafa mengine kwa binadamu.
“Mpaka sasa Jeshi la Zimamoto na vyombo vingine vya ulinzi na usalama vipo katika eneo hili kuendelea na hatua za kuhakikisha kama waliojeruhiwa ni hao tu ama kuna ziada, lakini Serikali imechukua hatua kwa wale wote waliojeruhiwa hatua za matibabu zinaendelea” amesema DC James.